NJOMBE-Kituo cha Afya Igagala kilichopo Kata ya Ulembwe, Halmashauri ya Wilaya ya Wanging'ombe tarehe 11 Agosti 2026 kimeanza kutoa rasmi huduma za dharura za uzazi salama, ikiwa ni hatua muhimu katika kuboresha huduma za afya kwa wananchi wa eneo hilo na maeneo ya jirani.
Katika siku ya kwanza ya kuanza kwa huduma hizo, kituo hicho kimefanikiwa kumhudumia mama aliyefanyiwa upasuaji wa kujifungua na kufanikiwa kupata mtoto wa kiume mwenye uzito wa kilogramu 3.2. Mtoto huyo alilia mara baada ya kuzaliwa, huku mama na mtoto wote wakiendelea vizuri bila kuonesha changamoto yoyote kiafya.
Wananchi na Uongozi wa kituo wametoa shukrani za dhati kwa serikali, inayoongozwa na Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, kwa kuendelea kuwekeza katika sekta ya afya na kuwezesha upatikanaji wa huduma bora za afya kwa wananchi kwa lengo la kuokoa maisha ya akinaamama na watoto.
