DAR-Bodi ya Mikopo ya Wanafunzi wa Elimu ya Juu (HESLB) imeongeza kwa siku 14 muda wa kuwasilisha maombi ya mikopo kwa wanafunzi wanaotarajia kusoma katika mwaka wa masomo 2026/2027.
Kwa mujibu wa tangazo lililotolewa na Mkurugenzi Mtendaji wa HELSB, Dk Bill Kiwia, muda wa mwisho wa kuwasilisha maombi ya mkopo umeongezwa kutoka Agosti 31 hadi Septemba 14, 2026.
HESLB imesema hatua hiyo imechukuliwa ili kuwapa fursa waombaji ambao, kwa sababu mbalimbali, hawakuweza kukamilisha na kuwasilisha maombi yao ndani ya muda uliokuwa umewekwa awali.
Bodi ilianza kupokea maombi ya mikopo kwa wanafunzi kwa njia ya mtandao tangu Juni 19, 2026, kwa ajili ya mwaka wa masomo 2026/2027.
Katika tangazo hilo, HESLB imewataka waombaji ambao tayari wamejisajili katika mfumo lakini hawajakamilisha mchakato wa maombi kuhakikisha wanakamilisha na kuwasilisha maombi yao kabla ya muda huo kuisha.
Hata hivyo, Bodi imesisitiza kuwa hakutakuwa na nyongeza nyingine ya muda baada ya Septemba 14, 2026, hivyo waombaji wametakiwa kutumia kikamilifu siku 14 zilizoongezwa kukamilisha maombi yao.
