KILIMANJARO-Septemba 3,2026 ofisi Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU) Wilaya ya Siha imefungua na kushinda shauri la jinai Na. 19847/2026 ikiwa ni Jamhuri ya Muungano wa Tanzania dhidi ya Bw. Oscar Timotheo Kiwale ambaye alikuwa Meneja wa Mradi wa Maji Magadini Makiwaru.
Shauri hilo limesikilizwa katika Mahakama ya Wilaya ya Siha mbele ya Mhe. Elibahati Petro, Hakimu Mkazi Mfawidhi na limeendeshwa na Mwendesha Mashtaka wa Serikali,Bw.Bernard Ndamallya
Bw. Oscar ameshtakiwa kwa kosa la kupokea hongo chini ya kifungu cha 15 (1) (a) (2) na (3) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Sura ya 329 Marejeo ya mwaka 2023.
Akiieleza Mahakama Bw. Ndamallya amesema kuwa, Hospitali ya Charlotte iliunganisha maji kinyemela na baada ya ukaguzi kufanyika hospitali hiyo ilitakiwa kulipa faini kiasi cha Shilingi 5,000,000 kwa kosa hilo.
Mnamo Aprili 9, 2026 mshtakiwa alipokea fedha kiasi cha Shilingi 900,000 kutoka kwa Mhasibu wa Hospitali ya Charlotte ili asitoze faini iliyostahili kulipwa.
Mnamo Septemba 3, 2026 mtuhumiwa alifikishwa mahakamani na alikiri kosa, hivyo Mahakama ilimtia hatiani na kumhukumu kulipa faini ya Shilingi 500,000 au kutumika kufungo cha miaka mitatu gerezani.
Vilevile Mahakama ilitoa amri kwa mshtakiwa kulipa Shilingi 900,000 kwa mhanga ambaye ni Magadini Makiwaru Water Supply Trust ndani ya siku saba kuanzia tarehe ya hukumu.
Mshtakiwa alitekeleza kulipa malipo ya faini zote kama ilivyoelekezwa na Mahakama siku hiyo hiyo ya hukumu na aliachiwa huru.
Tags
Habari
Mahakamani Leo
Meneja Mradi wa Maji
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)
TAKUKURU Tanzania
