Tanzania na POSCO International wajadili uendelezaji uwekezaji wa kimkakati sekta za madini,nishati na kilimo

SEOUL-Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar ameongoza ujumbe wa Tanzania, akiambatana na Waziri wa Mawasiliano na Teknolojia ya Habari, Mhe. Angellah Kairuki katika mkutano na watendaji wa kampuni ya POSCO International jijini Seoul Jamhuri ya Korea Kusini ambapo pamoja na mambo mengine, wamejadili namna ya kuendeleza fursa za uwekezaji wa kimkakati katika sekta za madini,nishati na kilimo.
Mkutano huo umesisitiza dhamira ya pamoja ya kuimarisha uhusiano wa kiuchumi na kuifanya Tanzania kuwa kituo kikuu cha shughuli za POSCO barani Afrika.

Majadiliano yalijikita katika maendeleo ya mradi wa grafiti wa Mahenge, ambao kwa sasa uko katika hatua ya mwisho ya ongezeko la mtaji na unatarajiwa kukamilika mwaka huu.
Pande zote mbili zimekubaliana kuhusu umuhimu wa miradi muhimu ya miundombinu, ikiwemo ujenzi wa barabara na ununuzi wa mabehewa ya reli, ili kuunga mkono mnyororo wa thamani wa madini. Miradi hii inatekelezwa kwa ushirikiano na Mfuko wa Ushirikiano wa Maendeleo ya Kiuchumi (EDCF) na Benki ya Exim ya Korea.

Mbali na mradi wa Mahenge, ujumbe wa Tanzania umewasilisha mpango mpana wa ushirikiano uliopanuliwa ikiwemo kuongeza thamani ya madini, kuendeleza viwanda vya kusindika nikeli, kobalti, na shaba, hasa katika mkoa wa Dodoma.
Miradi mingine iliyopendekezwa ni pamoja na uwekezaji katika uzalishaji wa mafuta ya mawese, utengenezaji wa mbegu ili kupunguza utegemezi wa uagizaji, na usimamizi wa mashamba makubwa, ubunifu wa kidijitali na viwanda, kushirikiana katika akili unde (AI) ya viwandani, roboti, na uchambuzi wa kidijitali.

Kwa upande wake, Makamu wa Rais Mtendaji wa POSCO international, Bw. Jae Sung Lim, ameitaja Tanzania kama mmoja wa washirika wao watano wakuu wa kimkakati barani Afrika na Ili kurahisisha uhusiano huo unaokua, Kampuni hiyo imetangaza mipango ya kuanzisha ofisi ya uwakilishi nchini Tanzania, ikihama kutoka muundo wa sasa wa usimamizi unaoendeshwa kutoka Afrika Kusini.
Mkutano huo ulihitimishwa kwa pande zote mbili kukubaliana kudumisha mawasiliano ya karibu kupitia njia za kidiplomasia, ikiwemo Ubalozi wa Tanzania mjini Seoul, ili kuhakikisha utekelezaji wa haraka wa mipango hiyo ya kimkakati.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

Know matter how large or small your business is, advertising here