Timu ya Manispaa ya Kinondoni, KMC FC imemaliza maandalizi yake ya mchezo wa mzunguko wa sita dhidi ya Timu ya Costal Union ya Tanga mchezo utakaopigwa katika Dimba la Uhuru jijini Dar es Salaam, anaripoti Christina Mwagala (KMC FC).
Kaimu Kocha wa timu hiyo,Habibu Kondo amesema kuwa, kikosi hicho kwa sasa kimefanya maandalizi ya kutosha kwa asilimia kubwa na hivyo kipo tayari kwa mchezo huo wa kesho.
Kocha Habibu amesema,ana uhakika na maandalizi ambayo wameyafanya katika kipindi ambacho ligi ilisimama kwa muda na kwamba anakiamini kikosi hicho kuwa kitaleta matokeo mazuri katika mchezo wa kesho.
Ameongeza kuwa, katika mazoezi hayo, ametumia nafasi hiyo kurekebisha makosa madogo madogo ambayo yalijitokeza katika michezo mwili na hivyo kupelekea kupoteza na kwamba mechi ya kesho itakuwa na ushindi mkubwa.
" Kikosi kimefanya mazoezi ya kutosha tunaimani kuwa katika mchezo wa kesho tunakwenda kupata matokeo mazuri kama ilivyo kawaida ya KMC FC, kwa sababu uwezo wa kushinda mechi hiyo tunao kwa asilimia 100,"amesema Kocha Habibu.
Katika hatua nyingine, Mchezaji wa KMC FC ambaye alikuwa majeruhi kwa muda mrefu, Sadala Lipandike ameanza kufanya mazoezi mepesi na timu leo kutokana na afya yake kuimarika.
Sadala alikuwa anasumbuliwa na goti na kwamba hivi sasa ameanza kufanya mazoezi kwa ajili ya kujiandaa na michezo mingine ya Ligi Kuu soka Tanzania Bara.



