Wagonjwa wapya wa saratani waongezeka Tanzania

Tanzania kuna ongezeko la wagonjwa wapya wa Saratani wapatao 50,000 na inakadiriwa kuwa, ifikapo mwaka 2030 kutakuwa na ongezeko la asilimia 50 ya wagonjwa wapya wa saratani,anaripoti Catherine Sungura (WAMJW) Dodoma.
Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima (kushoto).

Hayo yameelezwa na Waziri wa Afya, Maendeleo ya Jamii, Jinsia, Wazee na Watoto Dkt. Dorothy Gwajima wakati wa uzinduzi wa idara ya magonjwa ya saratani,huduma za patholojia na mkataba wa mteja kwenye Hospitali ya Benjamin Mkapa.

Dkt. Gwajima amesema kuwa ongezeko hilo kwa mujibu wa Takwimu za Shirika la Umoja wa Mataifa linaloshughulika na Tafiti za Saratani (IARC) na kuongeza kuwa Takwimu za hapa nchini za 2018 zinaonyesha kuwa idadi ya wagonjwa wapya wa Saratani ni 14,028 sawa na asilimia 33.3 ya wagonjwa wote nchini.

“Saratani kama moja ya magonjwa yasiyo ya kuambukiza inashika nafasi ya tano kwa wanaume na ya pili kwa wanawake kwa kusababisha vifo vitokanavyo na magonjwa yasiyo ya kuambukiza nchini. 

Kwa ujumla Saratani zinazoongoza kwa wanawake ni mlango wa kizazi na Saratani ya Matiti. Kwa wanaume, Saratani zinazoongoza ni Saratani za Tezi Dume, Koo pamoja na Kichwa na Shingo.

Aidha, Dkt. Gwajima amesema Magonjwa ya Saratani yanatibika iwapo tu mgonjwa atawahi kupata tiba katika Vituo vya Afya vinavyotoa huduma hiyo. Zaidi ya asilimia 75 ya wagonjwa wa Saratani hufika katika Vituo vya Matibabu wakiwa wamechelewa sana na kuwawia vigumu madaktari kutibu na kuponya ugonjwa huo. 

“Nitoe rai kwa wananchi, tujenge tabia ya kupima afya zetu mara kwa mara ili ikibainika kuwa tuna changamoto za kiafya basi tuanze matibabu bila kuchelewa”Alisisitiza Dkt. Gwajima

Aidha, amesema Serikali kwa kushirikiana na wadau na mashirika yasiyo ya Kiserikali imeendelea kuhakikisha inapambana na magonjwa ya saratani, ambapo katika kukabiliana na hilo Serikali imefunga mashine mbili za kisasa za tiba ya saratani kwa njia ya mionzi aina ya LINAC katika Taasisi ya Saratani ya Ocean Road ambazo zimeanza kutoa huduma tangu Septemba, 2018. 

Dkt. Gwajima aliongeza kuwa Serikali imeanzisha vituo takribani 624 ambavyo huweza kugundua na kutibu mapema saratani ya mlango wa kizazi.

Hata hivyo Dkt. Gwajima alifurahishwa na wataalamu wazawa wa Hospitali ya Benjamin Mkapa na wale wa Chuo Kikuu Dodoma kwa kujituma, kuwajibika na kuthubutu kuanzisha na kutoa huduma za kibobezi katika upandikizaji wa Figo. 

“Wagonjwa 16 wamepandikizwa Figo ndani ya kipindi cha miaka mitatu, kati yao wagonjwa 5 wamepandikizwa na wataalamu wetu wazawa. Hakika hili ni jambo la kijasiri kwani mmesaidia kupunguza mzigo wa gharama kwa Serikali na kwa Wananchi ambao walilazimika kufuata huduma hii nje ya nchi’.

Hata hivyo amesema uwepo wa Kitengo cha Patholojia ni faraja pia katika kuharakisha matibabu kwani hapo awali ilibidi sampuli zipelekwe Dar es Salaam ili kubaini kama ni saratani au la. Utaratibu huu ulikuwa unachelewesha kupata kwa zaidi ya wiki moja hadi mbili.

"Sampuli inatolewa na majibu yanatoka ndani ya kipindi kifupi na wanaobainika kuwa na saratani wanaanzishiwa tiba mapema. Vitengo hivi viwili lazima vifanye kazi kwa karibu kwani vinategemeana sana".

Naye Mkurugenzi wa Hospitali ya Benjamin Mkapa Dkt. Aliphonce Chandika amesema takwimu za shirika la IARC chini ya WHO zinaonyesha kwamba mwaka 2018 jumla ya watu 18.1 waligundulika kuwa na aina mbalimbali za saratani duniani,kati yao watu milioni 9.6 walifariki kutokana na magonjwa ya saratani.

Dkt. Chandika amesema kuanzishwa kwa daftari maalum la kuratibu maradhi ya saratani kanda ya kati mwaka 2018,saratani ya malango wa kizazi ndio inaongoza kwa saratani zote zilizoratibiwa ikiwa na jumla ya wagonjwa 778 sawa na asilimia 32 ya saratani zote na asilimia 50 kwa saratani za wanawake huku saratani ya tezi dume ikiongoza kwa wanaume ambapo wagonjwa 265 waliratibiwa sawa na asilimia 39 kwa upande wa wanaume.

Dkt. Chandika ameongeza kuwa umri unaoathirika zaidi na maradhi hayo ni kati ya miaka 50 hasi 69 ambapo jumla ya wagonjwa 1089 sawa na asilimia 42.2 ya wagonjwa wote.

Serikali ilijenga Hospitali ya Benjamin Mkapa, yenye uwezo wa kutoa huduma bobezi na za kisasa kwa kiwango cha kimataifa katika magonjwa ya Figo, Moyo na Matibabu ya Saratani, ili kuwezesha upatikanaji wa huduma hizo hapa nchini na hivyo kupunguza idadi ya wagonjwa wanaopewa rufaa kwenda kupata matibabu haya nchi za nje kama India na Afrika Kusini.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news