MAJALIWA: TPA IMARISHENI USIMAMIZI WA ‘FLOW METER’

Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Kassim Majaliwa ameiagiza Mamlaka ya Bandari Tanzania (TPA) ihakikishe inaendelea kuimarisha usimamizi wa mitambo ya mita za upimaji wa mafuta (Flow Meter) ili kudhibiti upotevu wa mapato ya Serikali, anaripoti Mwandishi DIRAMAKINI (Dar es Salaam).
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akifafanuliwa jambo na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania Mhandisi Deusdedit Kakoko, wakati alipo kagua mfumo wa mitambo ya mita za mafuta, Kurasini Oil Jety (KOJ) kwenye Bandari ya Dar es Salaam. Machi 3, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Pia, Waziri Mkuu amesema Serikali inataka kuona makusanyo yote ya mapato kutoka katika bandari zote nchini yanayokusanywa na TPA yanaingia katika mfuko mkuu wa Serikali na kwamba haitakubali kubaki na mtu yeyote anayejihusisha na upotevu wake.

Waziri Mkuu ametoa maagizo hayo leo Machi 3, 2021 baada ya kukagua mitambo ya mita ya mafuta Kigamboni na Kurasini Oil Jety (KOJ) kwenye Bandari ya Dar es Salaam.

Hata hivyo, Waziri Mkuu amesema ameridhishwa na utekelezwaji wa maagizo na maelekezo mbalimbali aliyoyatoa katika vipindi tofauti kuanzia mwaka 2016 alipofanya ziara katika eneo la mitambo ya mita ya mafuta (Flow Meter) ya Kigamboni na KOJ.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akihoji jambo, wakati alipokagua mfumo wa mitambo ya mita za mafuta, uliyopo Kigamboni jijini Dar es salaam, baada ya kutembelea kituo hicho Machi 3, 2021. Kutoka kushoto ni Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi, Mhandisi. Dkt. Leonard Madaraka Chamuriho, Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Bandari Tanzania Mhandisi Deusdedit Kakoko na Mhandisi wa Idara ya Mafuta, Mamlaka ya Bandari Tanzania, Yona Malago. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Amesema kipindi hicho teknolojia iliyokuwa inatumika haikuwa nzuri sana na ilikuwa inaifanya Serikali kupoteza kiasi kikubwa cha mafuta na kusababisha mapato yaliyokuwa yakipatikana kuwa madogo, hivyo Serikali iliyopita ilifanya maamuzi ya kununua flow meter ya Kigamboni.

Waziri Mkuu amesema Serikali ya Awamu ya Tano imeendelea kuimarisha ununuzi wa mitambo hiyo kwa lengo la kuboresha bandari za Dar es Salaam, Tanga na Mtwara hasa kwenye sekta ya mafuta. ”Leo nimekuja kuona hatua sahihi tuliyofikia na nimeridhishwa na utekelezaji wake.”
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akikagua mfumo wa mitambo ya mita za mafuta, uliyopo Kigamboni jijini Dar es salaam, baada ya kutembelea kituo hicho Machi 3, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Amesema baada ya kuona mifumo ya upimaji si sahihi sana Serikali ilipendekeza vinunuliwe viwanja Kigamboni ili kujenga matenki ambayo yatapokea mafuta kutoka bandarini, licha kupimwa katika ‘flow meter’ yanapopelekwa kwa mteja yatapimwa tena kuhakikisha mteja anapata kiwango sahihi cha mafuta anachokihitaji.

”Nimefurahi kupata taarifa kwamba viwanja vimenunuliwa na sasa zabuni ya ujenzi wa matenki mapya inafanywa, tukishafika hapo Taifa litanufaika sana kuwa na mafuta mengi yaliyopo kwenye akiba yetu. Pia hata wateja wanaotaka mafuta watakuwa wanaagiza wakati wowote kulingana na mauzo waliyoyafanya na kiwango wanachokihitaji kwa wakati huo,”amesema.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akikagua mfumo wa mitambo ya mita za mafuta, uliyopo Kigamboni jijini Dar es salaam, baada ya kutembelea kituo hicho Machi 3, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Waziri Mkuu amesema matanki hayo yatatoa fursa kwa nchi jirani ambazo zinatumia bandari hiyo kuagiza mafuta kwani wataweza kuhifadhi mafuta yao na kuiwezesha bandari hiyo kufanya biashara ya mafuta ndani na nje ya nchi. Ameagiza zabuni ya ujenzi wa matanki hayo iharakishwe ili ujenzi uanze mara moja.

Kadhalika, Waziri Mkuu ameitaka Mamlaka ya Bandari iimarishe usimamizi wa ‘flow meter’ na pia inatakiwa ianzishe idara maalumu ya kuzisimamia katika bandari zote. Amesema watendaji wa idara hiyo ndio watakaowajibika kwenye utunzaji na utoaji wa huduma katika eneo hilo.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akimuuliza jambo Mhandisi wa Idara ya Mafuta, Mamlaka ya Bandari Tanzania, Yona Malago, wakati alipo kagua mfumo wa mitambo ya mita za mafuta, Kigamboni jijini Dar es salaam. Machi 3, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Awali, Mhandisi wa Idara ya Mafuta wa TPA, Mhandisi Yona Malago alimueleza Waziri Mkuu hatua zilizochukuliwa na TPA ili kuhakikisha ufanisi wa kushusha mafuta kupitia mita ya Kigamboni unafikiwa. ”Hatua ya awali ni ile iliyowezesha mita kufanyakazi bila kusimama na hatua ya pili ni kufanya ukarabati mkubwa wa mita ikiwemo kurekebisha machujio.”

Alitaja hatua nyingine zilizochukuliwa kuwa ni pamoja na kuweka wafanyakazi wenye sifa, vigezo na uwezo wa kusimamia mita hizo ikiwa ni pamoja na wahandisi, mafundi sanifu na mafundi mchundo wa umeme, mitambo na tehama na kufanya mafunzo kwa wafanyakazi wa TPA ambao wanasimamia utendaji wa mita hiyo.
Waziri Mkuu Kassim Majaliwa, akifafanuliwa jambo na Mhandisi wa Idara ya Mafuta, Mamlaka ya Bandari Tanzania, Yona Malago, wakati alipo kagua mfumo wa mitambo ya mita za mafuta, Kurasini Oil Jety (KOJ) kwenye Bandari ya Dar es Salaam. Machi 3, 2021. (Picha na Ofisi ya Waziri Mkuu).

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news