GGML YAREKEBISHA MIDOMO SUNGURA YA WAGONJWA 25

NA ROBERT KALOKOLA

Watu 25 ambao ni wagonjwa wanaosumbuliwa na ugonjwa wa mdomosungura kutoka maeneo mbalimbali yanayozunguka mgodi wa kuchimba Dhahabu wa Geita (GGML) wamenufaika na udhamini wa kulipiwa gharama zote kutoka kwa mgodi huo kufanyiwa upasuaji katika Hospitali ya Sekou Toure jijini Mwanza ili kurekebisha maumbile ya midomo yao.
Baadhi ya wanawake ambao ni wazazi na walezi wa watoto ambao wana ugonjwa wa midomo sungura wakiwa kwenye hafla ya kuagwa kwenda kutibiwa Hospitali vya Sekou Toure jijini Mwanza kwa ufadhili wa GGML.(Picha na Robert Kalokola).

Wagonjwa hao watafanyiwa upasuaji wa kurekebisha maumbile ya midomo yao kwa udhamini wa GGML kwa kushirikiana na Rafiki Surgical Mission kutoka Australia kwa kutoa gharama za matibabu,chakula,malazi ,usafiri na huduma nyingine zote wanazohitaji katika kipindi chote cha matibabu yao hadi kupona.

Akizungumza kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu wa GGML, Meneja Mwandamizi wa wa mgodi huo anashughulikia Afya ,usalama ,Mazingira na mafunzo, Dkt .Kiva Mvungi amesema mgodi huo unapeleka wagonjwa hao ikiwa ni mara ya 18 tangu ulipoanza kutoa ufadhili huo kwa watu wanaosumbuliwa na ugonjwa huo hasa ukanda wa Ziwa Viktoria.

Amesema kuwa, mpango huo ulianza mwaka 2002 na hadi sasa umeshasaidia kuwatibu watu 1,717 ambao wamefanikiwa kurekebishwa midomo yao na kuwa na maumbile kama watu wengine na kuondokana na matatizo waliyo kuwa wanapitia wakati ambao walikuwa hawajafanyiwa upasuaji.
Dkt. Kiva Mvungi ambaye ni  Meneja Mwandamizi kutoka GGML akizungumza katika hafla ya kuaga wagonjwa wa midomo sungura kwenda kutibiwa katika hospitali ya Sekou Toure jijini Mwanza. (Picha na Robert Kalokola).
Baadhi ya wanawake ambao ni wazazi na walezi wa watoto ambao wana ugonjwa wa midomo sungura wakiwa kwenye hafla ya kuagwa kwenda kutibiwa Hospitali vya Sekou Toure jijini Mwanza kwa ufadhili wa GGML. (Picha na Robert Kalokola).

Dkt.Kiva Mvunge ameongeza kuwa, chanzo cha ugonjwa huo hakijajulika japo inasemekana ni matokeo ya jeni na sababu za kimazingira na tatizo hilo lipo kwa wingi ukanda wa Ziwa Viktoria, hivyo mgodi huo unatoa ufadhili ili kurudisha matumaini na tabasamu kwa watoto na watu wazima kwa kugharamiwa matibabu ,malazi na usafiri kipindi chote wanapatiwa matibabu katika hospitali husika.

Ameongeza kuwa GGML ni mdau mkubwa wa sekta ya afya katika mkoa wa Geita na Taifa kwa ujumla na kuongeza kuwa katika kipindi cha mlipuko wa Uviko19 mgodi huo ulichangia Serikali kuu Bilioni 1.6 na Milioni 750 kwa mkoa wa Geita katika kupambana na Uviko 19,lakini mgodi umeisha tekeleza miradi zaidi ya 45 ya afya katika Halmashauri mbili ya Geita na Geita mji kupitia mpango wa uwajikaji wa kampuni kwa jamii (CSR).

Dkt Kiva Mvungi amefafanua kuwa mgodi huo kwa kushirikiana na serikali umeisha wekeza kiasi cha Bilioni 50 kwenye miradi ya maendeleo katika maeneo ya afya,elimu na miundombinu lakini mgodi huo umeweza kulipa zaidi ya Trilioni 3.9 fedha za kitanzania kama kodi tangu kuanza shughili zake mwaka 2000.
Mkuu wa Wilaya ya Geita Wilson Shimo akiwa kwenye picha ya pamoja na baadhi ya wazazi na walezi wa watoto walipata ufadhili wa matibabu kutoka GGML kwenda kutibiwa Hospitali ya Sekou Toure Jijini Mwanza. (Picha na Robert Kalokola).
Mkuu wa Wilaya ya Geita Wilson Shimo akiwa amebeba moja ya watoto wenye ugonjwa wa mdomo sungura waliopata ufadhili wa matibabu kutoka GGML.(Picha na Robert Kalokola).

Mkuu wa Wilaya ya Geita, Wilson Shimo amesema kutoa ufadhili huo wa matibabu ya upasuaji wa midomo sungura kwa wagonjwa hao uliofanywa na mgodi huo kwa kushirikiana na Rafiki Surgical Mission ni mwendelezo wa GGML kusaidia sekta ya afya katika wilaya hiyo na wananchi .

Mkuu wa Wilaya, Wilson Shimo amewapongeza wananchi waliojitokeza hadharani kuleta watoto wao kufanyiwa upasuaji na kuachana na imani potofu za kuwafisha ndani ya nyumba na kuendelea kupata matatizo bila kutibiwa.

Amewataka wananchi kuachana na tabia ya kuficha walemavu ndani hasa watoto badala yake wajitokeze kwa ajili kutibiwa kama watu hao 25 waliojitokeza na kupata ufadhili wa matibabu kutoka mgodi wa GGML kwa ajili ya kufanyiwa marekebisho ya midomo yao.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news