Waziri Mhagama:Serikali itapima utendaji kazi wa taasisi zake kielektroniki

NA JAMES K. MWANAMYOTO

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama amesema Serikali inaboresha Mfumo wa Uwazi wa Kupima Utendaji Kazi wa Taasisi unaojulikana kama Mfumo wa Mikataba ya Utendaji Kazi katika ngazi ya Taasisi za Umma kuwa wa kielektroniki ili utumike kupima utendaji kazi wa taasisi za umma nchini.
Akizungumza ofisini kwake Jijini Dodoma, Mhe. Jenista amesema, mfumo huo wa kielektroniki utawezesha makubaliano ya kimaandishi kati ya Serikali na Taasisi za Umma kuhusu malengo ambayo Taasisi husika itayatekeleza katika kipindi cha mwaka mmoja.

“Malengo yaliyomo ndani ya Mkataba yatakuwa na vigezo, shabaha na viashiria vitakavyotumika kupima utendaji kazi wa Taasisi kila mwisho wa mwaka. Mkataba huu unalenga kuimarisha dhana ya utendaji unaojali matokeo, kuboresha utoaji wa huduma bora kwa wananchi, na kuongeza uwajibikaji wa viongozi katika Taasisi za Umma,” Mhe. Jenista amefafanua.

Mhe. Jenista ameongeza kuwa, Mfumo huo wa kielektroniki ukikamilika utatumika kulinganisha na kushindanisha utendaji wa taasisi na kutoa tuzo za utendaji bora kwa taasisi zenye utendaji mzuri kila mwaka.

Akizungumzia faida za Mfumo huo, Mhe. Jenista amesema utaongeza uwajibikaji katika utekelezaji wa Sera, Mikakati na Vipaumbele vya Taasisi, Sekta na Taifa kwa ujumla ikiwa ni pamoja na kuboresha utoaji huduma kwa umma, kuimarisha utamaduni wa utendaji unaojali matokeo na kuleta matumizi bora ya rasilimali za Umma.

Aidha, Mhe. Jenista amewataka Makatibu Wakuu na Watendaji Wakuu wote wa Taasisi za Umma kuendelea kusimamia utekelezaji wa mfumo huu kikamilifu na wahakikishe wanatenga bajeti kwa ajili ya kusimamia utekelezaji wake katika Taasisi wanazoziongoza.

Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora imejipanga vizuri kujenga na kusimamia mifumo yenye tija kupitia sekta ya Utumishi wa Umma.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news