Waziri Dkt.Kijaji:Watanzania muwe tayari kupokea wawekezaji kutoka UAE waliosaini hati za makubaliano 37

NA MWANDISHI MAALUM

WAZIRI wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara (Mb), Mhe. Dkt.Ashatu Kijaji amewaasa watendaji na wananchi kwa ujumla kuwa tayari kuwapokea wawekezaji kutoka Umoja wa Falme za Kiarabu (UAE) waliosaini mikataba 37 yenye thamani ya takribani trilioni 20 na ajira zaidi ya 200,000, ambao wanatarajiwa kuingia nchini kuanzia wiki ya pili ya mwezi Machi 2022 kwa ajili ya utekelezaji wa makubaliano hayo bila kuwakwamisha katika ngazi yeyote husika.
Dkt. Kijaji ameyasema hayo wakati akiongea katika kipindi cha Jambo Tanzania cha TBC1 na  Asubuhi Hii cha TBC Taifa vinavyorushwa na Shirika la Utangazaji Tanzania (TBC) leo Machi 3, 2022 kuhusu mafanikio yaliyopatikana kutokana na ushiriki wa Tanzania katika Maonesho ya Expo 2020 Dubai yaliyoanza Oktoba 1, 2021 hadi Machi 31, 2022 na utayari wa Watanzania kupokea uwekezaji huo utakaotoa fursa mbalimbali za kiuchumi na kijamii.

Aidha, Dkt. Kijaji amefafanua kuhusu hati hizo 37 zilizofanyiwa uchunguzi na kupitiwa na Mwanasheria Mkuu wa Serikali kabla ya kutiwa saini kati ya wawekezaji kutoka UAE na Tanzania katika sekta mbalimbali za kiuchumi kuwa zinajumuisha Hati za Makubaliano katika Sekta ya Kilimo (11), Nishati nane (8), Usafirishaji tano (5), Mawasiliano nne (4), Ujenzi tatu (3), Madini mbili (2), Miundombinu moja (1), Maliasili moja (1), Afya moja (1) na Viwanda moja (1).
Akielezea zaidi kuhusu uwekezaji huo, Dkt. Kijaji amesema miongoni mwa Hati hizo zilizosainiwa kuna Makubaliano yanayohusu uendelezaji wa miradi mipya na inayoendelea mfano Mradi wa Shamba la Mkulazi unahusika na kilimo cha miwa na mnyororo mzima wa uzalishaji sukari ikiwemo sukari ya viwandani pamoja na uzalishaji wa nishati ya umeme kwa kutumia upepo na jua

Dkt. Kijaji pia amesema Serikali imeandaa Mkakati wa utekelezaji wa uwekezaji wa Hati hizo za makubaliano kwa kushirikiana na Taasisi mbalimbali zinazohusika pamoja na Sekta Binasfi. Aidha, Kituo cha Uwekezaji cha Tanzania kinachojumuisha Ofisi zote muhimu zinazohusika katika uwekezaji katika sehemu moja kimeanza kufanya usajili wa makampuni ya wawekezaji hao.

Vilevile, Waziri Kijaji alisema kuwa Tanzania imepata fursa ya kutangazwa katika jengo refu kuliko yote Duniani liitwalo Burj Khalifa lililopo katika Jiji la Dubai, kwa muda wa mwezi mzima wa Machi, 2022 bila gharama yoyote ambapo picha za vivutio mbalimbali vya Tanzania vitatangazwa katika jengo hilo.
Dkt. Kijaji pia ameeleza kuwa Hati hizo za Makubaliano kati ya Serikali ya Tanzania na UAE, na Sekta binafsi ya Tanzania na UAE zimepatikana wakati Maonesho ya Expo2020 Dubai ambapo Tanzania ni miongoni mwa nchi 192 zinazoshiriki Maonesho hayo chini ya uratibu wa Wizara ya Uwekezaji, Viwanda na Biashara, Wizara ya Biashara na Maendeleo ya Viwanda - Zanzibar kupitia Mamlaka ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TANTRADE).

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news