Dkt.Biteko ataka madini kuongeza amani Ukanda wa Maziwa Makuu

*Aipongeza ICGLR kwa kuichagua Tanzania kufanya Mkutano wa 20 wa Kamati ya Ukaguzi

NA STEVEN NYAMITI,KAGERA

WAZIRI wa Madini, Dkt. Doto Biteko amesema, Kamati ya Ukaguzi wa Madini ya Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) ina jukumu kubwa la kuhakikisha kuwa, madini yanayochimbwa katika nchi wanachama wa jumuiya hiyo yanakuwa chachu ya amani na si migogoro.
Dkt.Biteko ametoa rai hiyo leo Aprili 4,2022 wakati akifungua Mkutano wa 20 wa Kamati ya Ukaguzi wa Madini ya Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) ambapo Tanzania ni mwenyeji wa mkutano huo unaofanyika mjini Bukoba Mkoa wa Kagera.

"Tunataka tuyaone madini haya yanachangia kwenye kuongeza amani kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu, hayachangii vita na mapigano na hayachangii migogoro," amesema Dkt. Biteko.
Waziri wa Madini, Dkt. Doto Biteko akifuatilia kinachozungumzwa na Mwenyekiti wa Kamati ya Ukaguzi wa Madini kabla hajafungua mkutano huo leo.

ICGLR inaundwa na nchi 12 ambazo ni Angola, Burundi, Jamhuri ya Afrika ya Kati, Jamhuri ya Congo, Jamhuri ya Kidemokrasia ya Congo, Kenya, Uganda, Rwanda, Jamhuri ya Sudan Kusini, Sudan, Tanzania na Zambia.

Amesisitiza kuwa, Tanzania ikiwa miongoni mwa wanachama wa ICGLR itaendelea kuhakikisha madini yanayochimbwa katika nchi zetu hayageuki kuwa nyenzo ya kufadhili uhalifu.
Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko akiwa na wajumbe kutoka nchi mbalimbali katika Mkutano wa 20 wa Kamati ya Ukaguzi wa Madini ya Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) mkoani Kagera.

Dkt.Biteko ameeleza kuwa, kikao hicho ni cha Kamati ya Ufuatiliaji wa Madini yanayozalishwa kwenye Ukanda wa Maziwa Makuu ambapo kamati hiyo ina jukumu la kufuatilia madini yanakochimbwa ili kusaidia kuleta faida kwenye nchi husika na kuongeza amani.

Akizungumzia umuhimu wa kamati hiyo amesema, madini ya Bati yanayochimbwa Kyerwa na maeneo mengine ili yaweze kuuzwa kwenye masoko ya nje lazima yawe na cheti cha uhalisia wa kule ulipoyatoa.

Dkt.Biteko amesema, kama hayana hicho cheti madini hayo hayajulikani na hayawezi kuingia kwenye soko.
Mjumbe wa Mkutano wa 20 wa Kamati ya Ukaguzi wa Madini ya Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu kutoka Wizara ya Madini, Bw. Mathias Abisai akifuatilia ufunguzi wa mkutano huo mkoani Kagera.

Kwa upande mwingine, Dkt. Biteko amesema, mkutano huo ni muhimu kwa Tanzania hususani kwa wachimbaji huku akisisitiza wachimbaji wachimbe kwa kuzingatia Sheria na Utaratibu uliowekwa.

"Serikali imeweka mazingira mazuri sana na Rais wetu anasisitiza kila ambaye anahitaji kuchimba achimbe bila matatizo. Lakini utoroshaji wa madini hauwezi kuvumiliwa," ameongeza.
Mwenyekiti wa Kamati ya Ukaguzi wa Madini ya Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu Fr. Dkt. David Luhaka akizungumza wakati akimkaribisha Waziri wa Madini kufungua mkutano huo.

Naye, Mwenyekiti wa Kamati ya Ukaguzi wa Madini ya Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR), Fr. Dkt. David Luhaka amesema kuwa, mkutano huo umelenga kuwakutanisha pamoja wakaguzi wa madini wa jumuiya hizo ili kuzungumzia mambo mbalimbali yanayojitokeza na kutolea ufafanuzi.
Waziri wa Madini Dkt. Doto Biteko akiwa na wajumbe kutoka nchi mbalimbali katika Mkutano wa 20 wa Kamati ya Ukaguzi wa Madini ya Jumuiya ya Ukanda wa Maziwa Makuu (ICGLR) mkoani Kagera.

Aidha, Fr. Dkt. Luhaka amesema kuwa, kamati hiyo itatembelea shughuli za uzalishaji wa madini katika Mkoa wa Kagera ili kujifunza vitu vinavyofanyika katika maeneo hayo na kutoa mapendekezo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news