Waziri Dkt.Mabula,Meneja Mkazi wa Tembo Nickel wateta

NA MUNIR SHEMWETA-WANMM

WAZIRI wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe.Dkt.Angeline Mabula amekutana na kufanya mazungumzo na Meneja Mkazi wa Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Nickel Tembo Nickel Corporation Ltd, Benedict Busunzu.
Meneja Mkazi wa Kampuni ya Tembo Nickel Corporation Ltd, Benedict Busunzu akifafanua jambo kwa Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mhe.Dkt Angeline Mabula walipokutana jijini Dodoma Juni 15, 2022.(PICHA NA WIZARA YA ARDHI).

Mapema mwaka 2021 Serikali ilitiliana saini mkataba na Kampuni ya LIZ Nickel ya Uingereza kwa ajili ya uchimbaji wa madini ya Nickel Kabanga mkoani Kagera, pamoja na ujenzi wa kiwanda cha kuchenjulia madini mbalimbali kinachojengwa Kahama, Shinyanga.

Utiaji saini wa mkataba kati ya Serikali ya Tanzania na Kampuni ya LIZ Nickel kuliwezesha kuanzishwa kampuni ya pamoja inayoitwa Tembo Nickel Corporation Ltd ambayo ni kampuni ya ubia.

Akizungumza mkoani Dodoma, Meneja Mkazi wa Kampuni ya Tembo Nickel, Busunzu alimueleza Waziri wa Ardhi kuwa kampuni yake imejipanga vizuri kwa ajili ya kuanza mradi wa uchimbaji madini ya Nickel huko Kabanga, Ngara mkoani Kagera.

Alisema, hatua ya kwanza waliyochukua ni kuwaelimisha wananchi wanaoishi eneo la mradi ili kuwajengea ufahamu kwa lengo la kuepuka migogoro wakati wa ulipaji fidia kwa wale wananchi watakaohamishwa kupisha mradi.

‘’Tumetumia muda mrefu kuwaelimisha wananchi kabla ya kuanza uzalishaji wa Nickel hii itatusaidia kuepuka migogoro wakati wa zoezi la ulipaji fidia kwa wale wananchi watakaohamishwa kupisha mradi,’’alisema Busunzu.
Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi Mhe. Dkt.Angeline Mabula akizungumza na Meneja Mkazi wa Kampuni ya Uchimbaji Madini ya Tembo Nickel Benedict Busunzu jijini Dodoma Juni 15, 2022. Kulia ni Meneja Uhusiano na Mawasiliano wa Tembo Nickel Corporation Ltd, Sauda Simba.

Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Dkt.Angeline Mabula alimueleza Meneja huyo mkazi wa Kampuni ya Tembo Nickel Corporation kuwa, uamuzi wa kutoa elimu kwa wananchi ni nzuri kwani utasaidia kuepuka migogoro hasa ile ya fidia kabla ya kuanza mradi.

‘’Hatua mliyochukua ya kutoa elimu mapema ni nzuri na itasadia kuondoa migogoro wakati wa zoezi la ulipaji fidia na ni vizuri pia mkafanya utaratibu wa kuthaminisha eneo lote la mradi kama ilivyofanyika kwenye mgodi wa Nyanzaga kule Sengerema,’’ alisema Dkt.Mabula.

Matokeo ya awali ya uzalishaji madini ya Nickel Kabanga wilayani Ngara mkoani Kagera, yanaonesha kutakuwa na wastani wa mauzo yenye thamani ya dola za marekani zaidi ya milioni 664 kwa mwaka.

Katika makubaliano ya mkataba wa Mradi huo Serikali itakuwa na umiliki usiopungua asilimia 16 ya hisa za mradi zisizolipiwa na zisizopungua thamani, hivyo kupata gawio kwenye faida zitakazopatikana baada ya kulipa kodi zote stahiki za serikali.

Utafiti uliofanywa na Serikali ya Tanzania kuanzia mwaka 1976 hadi1979 ulibaini kuwepo kwa madini ya Nickel katika mwamba unaoanzia eneo la Msongati nchini Burundi hadi Kabanga ambapo kiasi kikubwa cha Nickel kinapatikana Kabanga na ni ya daraja la kwanza.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news