Dakika 150 zatumika kuwamegea Watanzania siri, fursa zilizopo SADC

NA DIRAMAKINI

MKUTANO maalum na muhimu ulioangazia juu ya kukua kwa Diplomasia ya Uchumi na Fursa za Kiuchumi zinazopatikana nchi za Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika (SADC) umetoa mwelekeo thabiti ambao licha ya kuainisha maeneo zilipo fursa, pia umeonesha ni kwa namna gani Watanzania wakitumia njia sahihi wanaweza kunufaika kupitia uwekezaji wao nje ya mipaka.

Hayo yamethibitishwa leo Julai 9, 2022 kupitia mkutano huo ulioratibiwa na Watch Tanzania kupitia Mtandao wa Zoom ambao umerushwa na vyombo mbalimbali vya habari huku washiriki mbalimbali wakiwemo wanadiplomasia wakichangia mjadala kwa udhamini wa Benki ya Maendeleo ya Kilimo Tanzania (TADB) na Airtel Tanzania. Waliyosema washiriki wa mkutano huo; 

BALOZI WA NAMIBIA MHE.DKT. MODESTUS F. KIPILIMBA

"Ukubwa wa Namibia ni kilomita za mraba 840,000 huku Tanzania ikiwa na kilomita za mraba 945,000, hivyo hazitofautiani sana japo idadi ya watu Namibia ni milioni 2.5 tu;"Shughuli wanazojihusisha zaidi ni uchimbaji na uuzaji wa madini aina ya Almasi kwa asilimia 28.1 pia kuna Cooper na Uranium huku shughuli za uvuvi pia zinafanyika hasa uvuvi wa kina kirefu hivyo fursa ni nyingi sana Watanzania wanakaribishwa,"amesema Balozi Modestus. 

MKURUGENZI WA MIUNDOMBINU YA UCHUMI NA HUDUMA ZA JAMII ELIABI KHALID CHODOTA

"Zamani ukiangalia mazungumzo mengi kwenye mikutano ya SADC viongozi walikuwa wanazungumzia sana masuala ya ukombozi wa nchi, ila sasa hivi mwelekeo umebadirika kidogo vikao vingi vinazungumzia namna ya kuleta maendeleo baina ya nchi na utunzaji wa amani;
"Nchi za Jumuiya ya Afrika Mashariki wana mpanago wa kuwa na reli itakayounganika na reli ya TAZARA inayounganisha nchi za SADC kusudi ziweze kushirikiana kwenye masuala ya kimaendeleo na fursa zilizopo kwenye jumuiya hizi mbili,"amesema Chodota. 

MKURUGENZI MKUU WA SHIRIKA LA BANDARI TANZANIA PLASDUCE M. MBOSSA 

"Bandari yetu ya Tanzania imekuwa ni lango kuu la nchi zilizopo kwenye umoja wa nchi za SADC, tumekuwa tukishirikiana na nchi hizi kwa ukaribu mkubwa na tunashukuru Uongozi wa Rais wetu Samia (Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan) unazidi kuimarisha mahusiano hayo;
"Mwaka wa fedha wa 2019-2020 bandari yetu ilihudumia mizigo ya tani 6.6 milioni huku mwaka wa fedha uliyofuata 2021-2022 tulihudumia mizigo tani milioni 7.1 hili likiwa ni ongezeko la asilimia 17 kwa takwimu hizi zinaonesha kwamba kadri siku zinavyozidi kwenda idadi ya mizigo inayopitia bandarini inazidi kuongezeka hivyo ni faida kwetu sisi kama taifa,"amesema Mbossa.

BALOZI WA TANZANIA NCHINI MSUMBIJI BALOZI MHE.RET.CGP. PHAUSTINE MARTIN KASIKE 

"Tanzania na Msumbiji imekuwa na mahusiano mazuri na kwa kweli ubalozi wetu wa Tanzania hapa Msumbiji umekuwa na vikao mbalimbali na wafanyabiashara mbalimbali na taasisi husika (chamber of commerce) kujadili fursa mbalimbali zilizopo na kujaribu kuzitangaza nchini Tanzania kusudi Watanzania wanufaike nazo;
"Hapa nchini Msumbiji fursa zilizopo ni nyingi sana, nchi inauhitaji wa bidhaa za viwandani kama nguo (vitenge na kanga) pia inauhitaji wa bidhaa za kemikali (vipodozi), chakula na nafaka, viungo vya chakula na mahitaji mengi mengi tu hivyo fursa zipo nyingi sana,"amesema Balozi Kasike. 

MKURUGENZI BIASHARA, UWEKEZAJI NA SEKTA ZA UZALISHAJI BERNARD DAMAS HAULE

"Mkataba wa SADC (Jumuiya ya Maendeleo Kusini mwa Afrika) umewezesha kuunda soko huru la bidhaa na kuondoa ushuru wa forodha ambao umekuwa kikwazo kwa muda mwingi sana na hii itachochea ukuzaji wa viwanda ;
"Pia ndani ya mkataba huu wa SADC umeweza kuchochea uwekezaji wa nje na hivyo nchi za jumuiya ya Afrika Kusini zinapaswa kutengeneza mazingira rafiki kwa wawekezaji kuja kuwekeza kwenye nchi husika pale wanapoona fursa,"amesema Haule.

BALOZI WA TANZANIA NCHINI MALAWI MHE. HUMPHREY POLEPOLE 

"Kwa sasa Tanzania ndio kwa kiasi kikubwa inaleta bidhaa zake hapa nchini Malawi hivyo na sisi kama balozi tunaunda mikakati mbalimbali kusudi Wamalawi na wao walete bidhaa zao nchini, lakini serikali yetu chini ya Rais Samia (Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan) inajitahidi kwa asilimia kubwa kuendelea kuendeleza mahusiano baina ya hizi nchi mbili;
"Fursa huku Malawi zipo nyingi sana mfano mzuri Malawi wanalima sana zao la Soya ambalo linahitajika Tanzania, pia Malawi wanalima sana karanga zenye maganda mekundu ambazo kwa Tanzania zinahitajika kimkakati sana,"amesema Balozi Polepole. 

BALOZI WA TANZANIA ZIMBABWE MHE.PROF. EMMANUEL MBENNAH 

"Tanzania imekuwa bega kwa bega katika kushirikiana na nchi ya Zimbabwe katika upiganiaji wa uhuru tangu mwaka wa 1960 mpaka 1980 ambapo Zimbabwe ilipata uhuru; 
"Kupitia shirika letu la ndege la Air Tanzania limekuwa likifanya safari zake mara nne kwa wiki na hii imefanya idadi kubwa ya watalii kutoka Zimbabwe kuja Tanzania kuongezeka,"amesema. 

BALOZI WA TANZANIA NCHINI ZAMBIA MHE. HASSANI SIMBA YAHYA

"Mahusiano kati ya Zambia na Tanzania yamekuwa kwa muda mrefu sana, kwani waasisi wetu Mwalimu Nyerere na Kaunda walishirikiana kujenga misingi ya falsafa na kufanikiwa kuanzisha ushoroba wa Dar es Salaam ambao ni kati ya ushoroba uliofanikiwa sana barani Afrika; 
"Uchumi wa Tanzania unategemeana sana na uchumi wa Zambia, kwani tumekuwa tukishirikiana zaidi kwenye sekta ya uchukuzi, nisharti na viwanda,"amesema. 

MWENYEKITI MSAIDIZI CHAMA CHA WAMILIKI WA MALORI TANZANIA ELIAS LUKUMAY 

"Kusudi bandari yetu ya Dar es Salaam ipumue lazima lango la Tunduma liimarike zaidi ikiwezekana hata kuongezwa mageti kuliko kuwa na geti moja tu; 
"Kumekuwa na changamoto sana ya foleni kwenye lango letu la Tunduma, hivyo nashauri Serikali ione haja ya kufungua lango la Sumbawanga kusudi tupunguze msafara na idadi kuwa ya magari pale Tunduma,"amesema Lukumay. 

BALOZI WA TANZANIA NCHINI COMOROS MHE. PEREIRA A. SILIMA 

"Mahusiano kati ya Tanzania ni visiwa vya Comoros yamekuwepo muda sana na kumekuwa na historia ya kipekee na visiwa vya Zanzibar ambavyo vinaunga nchi ya Tanzania; 
"Fursa zinaopatikana visiwa vya Comoros ni nyingi sana visiwa hivi hinauhaba wa chakula na bidhaa zinazotokana na kilimo na vifaa vya ujenzi,"amesema. 

MKURUGENZI MAHUSIANO WA KAMPUNI YA BAKHRESA HUSSEIN SUFUIAN

"Kampuni ya Bakhresa ni moja ya kampuni za Kitanzania inayonufaika kwa kiasi kikubwa na umoja huu wa jumuiya ya SADC kwani jumuiya hii ina watu sio chini ya milioni 350 hivyo ni fursa kubwa mno kwetu. 

"Tumekuwa wawekezaji katika nchi nyingi za SADC, hivyo mahusiano mazuri ya nchi hizi yanatupa amani na utulivu kuendelea kuwekeza zaidi na kuiwakilisha zaidi nchi yetu katika mataifa mbalimbali,"amesema. 

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news