Walebanon wanavyoteswa na foleni ndefu za kununua mkate

NA DIRAMAKINI

TAIFA la Lebanon linaonekana kupitia kipindi kigumu zaidi kiuchumi, hali ambayo imesababisha maumivu kwa raia hususani pale wanapohitaji vyakula ikiwemo mikate.
Mwanaume akitoka kwenye duka la kuoka mikate akiwa na mfuko wa mkate wa bapa huku wengine wakiendelea kusubiri kwenye foleni, katika mji mkuu wa Beirut nchini Lebanon.

Kwa mujibu wa Shirika la Habari la AFP, Khalil Mansour ambaye ni miongoni mwa Walebanon anatakiwa kupanga foleni kwa muda mrefu kila siku ili tu kununua mkate kwa ajili ya familia yake na siku kadhaa hawezi kumudu chochote tena.

Katika nchi ambayo iliwahi kujivunia jina la utani la Uswisi ya Mashariki ya Kati kutokana na sekta yake ya benki inayostawi kabla ya shida ya kifedha mwaka 2019, uhaba wa kudumu wa chakula Lebanon umekuwa miongoni mwa vikwazo vikubwa kwa raia.

Lebanon ilishindwa kulipa deni lake la kitaifa mwaka 2020 na sarafu yake imepoteza karibu asilimia 90 ya thamani yake kutokana na kushamiri kwa huduma zisizo halali (black market).

Benki ya Dunia imetaja mzozo wa kifedha kuwa mbaya zaidi tangu karne ya 19 wakati Umoja wa Mataifa sasa unawachukulia Walebanon wanne kati ya watano kuwa wanaishi chini ya mstari wa umaskini.

Ikikabiliwa na matakwa kutoka kwa wakopeshaji wa kimataifa kwa ajili ya mageuzi ili kutibu maumivu kwa ajili ya kutolewa kwa msaada mpya, serikali inayokabiliwa na migogoro imelazimika kusitisha ruzuku kwa bidhaa muhimu zaidi ikiwemo ngano kiasi.

Licha ya hatua hiyo, bei ya mkate wa ruzuku imepanda,ni kama hakuna ruzuku, lakini kampuni za mikate zimeanza kusambaza chakula hicho kikuu kwa raia wengi nchini humo.

Mfuko wa mkate bapa wa Kiarabu unaofanana na chapati sasa unauzwa rasmi kwa pauni 13,000 za Lebanon (senti 43 za Marekani) katika masoko ambayo si halali inagharimu zaidi ya 30,000.

"Wiki iliyopita nilikaa bila mkate kwa siku tatu kwa sababu sina uwezo wa kulipa 30,000," Mansour mwenye umri wa miaka 48 alisema.

Kwa Mansour na Walebanoni wengi, kununua mkate kunamaanisha kusimama kwa saa nyingi kwenye foleni ndefu nje ya maduka ya kuoka mikate na wakati mwingine, wakati zamu yao inapofika, wanaooka mikate huishiwa na mikate.

“Leo nimepanga foleni kwa saa tatu, jana saa mbili na nusu. Nini tena?” Mansour alisema siku ya Ijumaa nje ya duka la kuoka mikate la Beirut.

“Lazima nilishe familia yangu. Nini kingine ninaweza kufanya?” aliuliza Mansour, ambaye hupata sawa dola 50 kwa mwezi (Shilingi 116,500 za Kitanzania) kufanya kazi katika duka la kuoka na kuuza mikate.

Mgawo

Makampuni mengi ya kuoka mikate yanapunguza uuzaji wa mikate kwa kifungashio kimoja au viwili kwa kila mteja, na kila mfuko una mikate sita ya bapa.

Mkate wa ruzuku mara nyingi hununuliwa kwa kiasi kikubwa na kuuzwa tena kwenye soko la mlango wa nyuma na wafanyabiashara wasiokuwa waaminifu. "Foleni zimekuwa mbaya zaidi katika wiki mbili zilizopita," alisema Mohammed Mehdi ambaye ni mmoja wapo wa wamiliki wa maduka ya kuokoa mikate na kuongeza kuwa;

"Tunakabiliwa na uhaba mkubwa." Mzee huyo mwenye umri wa miaka 49 alisema biashara ya kutengeneza mikate imekuwa kama kitanzi kwao.

"Baadhi ya wateja huja wakiwa na bunduki na visu," alilalamika. Vyombo vya habari vya Lebanon vinaripoti mara kwa mara mapigano yanayozuka kwenye maduka ya mikate, na hata risasi zinazofyatuliwa na wateja wakidai mkate zaidi.

Mathalani huko Taalbaya, Mashariki mwa Lebanon, mteja alivamia duka la kuoka mikate Jumanne akiwa na hasira kwa kushindwa kununua mkate zaidi, ripoti moja ilisema. Mteja alimsukuma mfanyakazi kisha akapora mkate, na kulazimisha jeshi kuingilia kati," iliongeza.

"Kinachotokea ni tusi...na ni ngumu zaidi kuliko uhaba wa petroli ambao uliikumba Lebanon mwaka jana," Mehdi alisema.

Kwa mujibu wa taarifa, Lebanon inaagiza asilimia 80 ya ngano yake kutoka Ukraine iliyokumbwa na vita, kulingana na takwimu za viwanda.

Lakini uwezo wa nchi hiyo wa kuhifadhi ngano ulipata pigo kubwa wakati mlipuko mbaya katika bandari ya Beirut mwezi Agosti 2020 ambao uliharibu sana maghala makuu ya nafaka nchini humo.

Serikali na kampuni za kuoka mikate zimebadilisha lawama kwa uhaba wa mkate. Kampuni za kuoka mikate zinatuhumu mamlaka zilizo na fedha taslimu kwa kushindwa kutoa unga wa kutosha wa ruzuku.

Wizara ya Uchumi inakanusha madai hayo na imezituhumu kampuni za kuoka mikate kwa kuhifadhi unga wa ruzuku ili kuutumia katika bidhaa ambazo hazijapewa ruzuku kama vile peremende (candy bar).

Mamlaka pia zinadai kuwa kuwepo nchini Lebanon zaidi ya wakimbizi milioni moja kutoka Syria iliyokumbwa na vita kunachangia kwa kiasi fulani kuporomoka kwa uchumi wa Lebanon.

Baadhi ya Walebanon wamefikia hatua ya kuwashutumu wakimbizi wa Syria kwa kununua mkate wa ruzuku ili kuuuza kwenye soko la mlango wa nyuma, na hivyo kuchochea chuki dhidi ya wakimbizi hao na kuwataka warudi nyumbani.

Kumekuwa na ripoti za baadhi ya maduka ya kuoka mikate kuweka foleni tofauti kwa Walebanon na Wasyria. Hii imesababisha Shirika la Umoja wa Mataifa la Kuhudumia Wakimbizi kueleza wasiwasi wake.

"Lebanon inashuhudia ongezeko la mivutano na uchochezi kati ya jamii tofauti, na kusababisha vurugu za mitaani, ikiwa ni pamoja na dhidi ya wakimbizi," UNHC inaeleza.

Makala hii imetafsiriwa na kuhaririwa na GODFREY NNKO,mhariri wa DIRAMAKINI kutoka Shirika la Habari la AFP,taarifa zote ni haki ya chanzo husika pamoja na picha.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news