NDANI YA KOKWA LA EMBE-4: Figisu zote zikome, mpira uwe pesa

NA LWAGA MWAMBANDE

UKITAKA kufahamu ukweli kuhusu kukua kwa soka la Tanzania, jaribu kuifuatilia kwa karibu Ligi Kuu ya NBC Tanzania Bara kupitia mitanange mbalimbali inayochezwa nchini.

Kama si kuridhika kwamba, soka limekua na linaendelea kukua, basi unaweza kutumia muda wako kuzishauri klabu kongwe hapa nchini kwa maana ya Simba SC na Yanga SC za jijini Dar es Salaam kukaa na kujitafakari, ili kuja na mbinu ambayo itaendelea kuwapa hadhi ya ukongwe wao.

La, si hivyo mwisho wa siku usishangae ukaona, timu changa zaidi ambazo zipo katika ligi hiyo au zinachipukia zikafanya mambo makubwa ya kushangaza ndani na nje ya nchi.

Ukongwe wa Simba na Yanga unapaswa kuwa na matunda chanya kwa kupenya zaidi anga za Kimataifa. Mshairi wa kisasa, Bw.Lwaga Mwambande anakushirikisha jambo muhimu kupitia shairi hapa chini;

1. Soka letu linakua, kama mpya ukurasa,
Kushangilia chagua, jipe mwenyewe ruksa,
Vipaji inaibua, wapya wazidi tikisa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

2. Mwamko wa mashabiki, nao ni muhimu hasa,
Amsha amsha tiki, inaongeza hamasa,
Kuvaa jezi mantiki, klabu zapata pesa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

3. Mwaka huu mwaka dume, kwa mpira wa kisasa,
Figisu zote zikome, mpira uwe ni pesa,
Na wa kubeti wakome, mechi zikiwanyanyasa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

4. Ligi ni mapema sana, ndiyo inaanza hasa,
Pengine twasema sana, tunapata tunakosa,
Ila jinsi tunaona, timu zetu bora hasa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

5. Chondechonde tunaomba, na tena hili twaasa,
Na mkwara tunachimba, kusifanyike makosa,
Tusijekitu kuumba, tukageuza kurasa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

6. Chama chetu cha mpira, mnatujenga kisasa,
Kama tungepiga kura, mwaupiga mwingi hasa,
Udhamini kuwa bora, ni nyie mmetikisa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

7. Ni vema kuhakikisha, sheria zang’ata hasa,
Hata kibidi kukesha, zibaki bila kudesa,
Kila anayechezesha, kuharibu si ruhusa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

8. Marefa mna dhamana, msijekuhongwa pesa,
Filimbi za konakona, mjue tutawatosa,
Tunajua tunaona, adhabu tutawanasa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

9. Kama kona iwe kona, msijefanya siasa,
Penati mkiziona, hata tano siyo kosa,
Tunatamani kuona, mechi bora bila visa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

10. Hili nalo tuliseme, linapunguza asusa,
Viwanja chipsi dume, wachezaji vyawatesa,
Hivyo ni bora vikome, vibaki vinavyonesa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

11. Sasa wito timu zetu, kwa Simba na Yanga hasa,
Pokeeni wito witu, mzidi ishi kisasa,
Jengeni viwanja vyetu, mtatengeneza pesa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

12. Mpira ajira kubwa, na tena ni ya kisasa,
Vijana wala ubwabwa, soka linalipa hasa,
Vya wadogo na wakubwa, vitalu anzisha sasa,
Ndani ya kokwa la embe, dudu laweza ingia.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.co m 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news