NMB HEKO KWA KUWEZESHA KILIMO: Kwa pesa ilizotenga, kilimo inanogesha nchini

NA LWAGA MWAMBANDE

SEPTEMBA 3, 2022 kupitia mjadala wa Kitaifa ulioandaliwa na Watch Tanzania kupitia Mtandao wa Zoom uliangazia juu ya maendeleo na fursa za kiuchumi katika mikoa ya Kaskazini mwa Tanzania ikijumuisha mkoa wa Tanga, Arusha, Kilimanjaro na Manyara.

Katika mjadala huo wa saa mbili, Meneja wa Kanda hiyo wa Benki ya NMB, Bw.Dismas Prosper aliweka wazi kuwa, benki hiyo tayari imeshatoa shillingi bilioni tatu kwa ajili ya wakulima wa zao la mihogo kule Handeni mkoani Tanga.

Hiyo ikiwa ni jitihada ya kuwezesha zao hilo la kibiashara kupanda thamani, pia katika mkoa wa Tanga wametoa shillingi bilioni sita kwa wakulima wa zao la mkonge.

Bw.Prosper alibainisha kuwa, kwa ujumla nchi nzima NMB imeshatoa mikopo ya shillingi trilioni 1.2 kwenye mnyororo wa kilimo, uvuvi na ufugaji, hii ni kuunga mkono juhudi za Serikali katika kuleta matokeo chanya katika sekta ya kilimo na sekta ya ufugaji nchini.

Mshairi wa kisasa, Bw.Lwaga Mwambande licha ya kupongeza hatua hiyo, anasema kuwa, huu ni mfano wa kuigwa ambao unapaswa kutekelezwa na wadau wengine nchini ili kuiwezesha sekta ya kilimo na ufugaji kanda zote nchini iweze kuleta matokeo chanya kwa jamii na Taifa kwa ujumla, ili kufahamu kwa kina unaweza kujifunza kupitia shairi hapa chini;


1.Benki NMBii, kwa kweli yafurahisha,
Ni ya nchi hii hii, ifanyayo yatukosha,
Kutoa haikawii, uchumi kuchangamsha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

2.Mikoa minne hii, Tanga, Manyara, Arusha,
Na Kilimanjaro hii, NMB yatisha,
Jitihada inatii, wananchi kuwezesha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

3.Kule mkoani Tanga, mazao inaboresha,
Handeni imejipanga, mihogo kuipaisha,
Kwa pesa ilizotenga, kilimo inanogesha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

4.Bilioni tatu hizo, zao hilo kuboresha,
Mihogo kwa pesa hizo, kwa biashara zatosha,
Tuvune liwe ni nguzo, kwa kipato cha kutosha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

5.Tena huko huko Tanga, benki moto imewasha,
Mkonge wa huko Tanga, wakulima kuwezesha,
Bilioni sita tenga, ili wazidi zalisha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

6.Jumla kwa nchi nzima, kilimo yakiwezesha,
Trilioni moja nzima, na juu yake zidisha,
Wavuvi wenye wanyama, wote inawawezesha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

7.Sasa chanya matokeo, benki inayafikisha,
Hii kwa maendeleo, inazidi kupandisha,
Haya mambo ya kileo, wala isije sitisha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

8.Kama wewe unalima, jambo la kufurahisha,
Mvuvi sishike tama, wapo wa kukuwezesha,
Mfugaji hili soma, ni zuri si la kutisha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

9.NMB kutenga, pesa za kuwawezesha,
Wale inaowalenga, nimeshawafahamisha,
Bilioni imetenga, mia mbili kukopesha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

10.Riba silimia tisa, sekta kuziwezesha,
Msijefanya makosa, fursa kuiyeyusha,
Hiyo kwenu ni hamasa, miradi kuizidisha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

11.Pia kujenga maghala, nchi nzima ya kutosha,
Mazao tunayokula, tutunze tukikausha,
Kesho yawe mbadala, kula na kusafirisha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

12.Na hii Bima ya Afya, kweli inafurahisha,
Wakulima wenye chafya, na magonjwa ya kutisha,
Wapate huduma afya, bila kujihangaisha,
NMBii heko, kwa kuwezesha kilimo.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news