NA DORINA G. MAKAYA
KAMATI ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini imeupongeza uongozi wa Shirika la Umeme nchini (TANESCO) na watumishi wa Kituo cha Kufua Umeme cha Kinyerezi II kinachozalisha umeme kwa kutumia gesi asilia na mvuke.
Ni kwa kudumisha usafi, kuendesha mitambo na kuikarabati kwa weledi pamoja na kuwa na mikataba ya muda mrefu ya upatikanaji wa vipuri kutoka kwa waunda mitambo.
Kituo cha Kufua Umeme cha Kinyerezi II, kinachozalisha umeme kwa kutumia Gesi Asilia na Mvuke chenye uwezo wa kuzalisha 240 MW kinavyoonekana pichani.Pongezi hizo zimetolewa na Mwenyekiti wa Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Nishati na Madini, Mhe. Dunstan Kitandula, baada ya kamati hiyo kutembelea Kituo hicho cha Kufua Umeme cha Kinyerezi II, kinachozalisha umeme kwa kutumia Gesi Asilia na Mvuke chenye uwezo wa kuzalisha 240 MW na kupata maelezo kutoka kwa uongozi wa TANESCO na wa kituo hicho Oktoba 13, 2022.

Aidha, Mhe. Kitandula, ameikumbushia TANESCO kuwa, kwa vile inajua muda wa matumizi ya mitambo iliyofungwa, ihakikishe inajiandaa kuweka mitambo mipya pindi mitambo iliyopo itakapokwisha muda wake.
Naye Mwakilishi wa Katibu Mkuu Wizara ya Nishati, Kamishna Msaidizi wa Masuala ya Gesi, Mha. Fakihi Mohamed, ameishukuru kamati hiyo kwa kutembelea Kituo hicho na kuwapatia maoni mazuri na ya kimkakati na kuahidi kuwa maoni hayo yatazingatiwa katika maandalizi na maboresho ya mikakati ya Wizara katika kuongeza kasi ya utendaji na ufanisi katika Sekta ya Nishati.
Vilevile, Mwakilishi wa Mkurugenzi Mtendaji wa Shirika la Umeme Tanzania, Mha. Athanasius Nangali, ameishukuru kamati hiyo kwa kutembelea kituo hicho na kuahidi kutekeleza maoni na mapendekezo ya Kamati hiyo ipasavyo.
Kamati hiyo ilitembelea sehemu mbali mbali za kituo hicho ikiwemo sehemu ya kupokea taarifa za uzalishaji wa umeme na uendeshaji wa mitambo kituoni hapo na sehemu ya kuhifadhi na kuchakata maji yanayotumika kuendesha mitambo ya kutengeneza umeme kwa mvuke, Oktoba 13, 2022.