Waziri Mhagama asisitiza umuhimu wa hatimiliki za kimila Meru

NA VERONICA MWAFISI

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama ametoa wito kwa wananchi wa Vijiji vya Karangai na Maweni, Halmashauri ya Wilaya ya Meru kutumia hatimiliki za kimila walizonazo kufanya shughuli za maendeleo ili kujikwamua kiuchumi.
Muonekano wa jengo la masijala ya ardhi lililojengwa na MKURABITA katika Kijiji cha Karangai, Kata ya Kikwe, Halmashauri ya Wilaya ya Meru mkoani Arusha lililozinduliwa na Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za MKURABITA katika Halmashauri hiyo.

Mhe. Jenista ametoa wito huo mara baada ya kukagua na kuzindua masijali za ardhi za Vijiji vya Karangai na Maweni katika Halmashauri ya Wilaya ya Meru mkoani Arusha zilizojengwa na Mpango wa Kurasimisha Rasilimali na Biashara za Wanyonge (MKURABITA).

Mhe. Jenista amesema MKURABITA imekuwa ikifanya kazi nzuri ya kurasimisha ardhi, lengo likiwa ni kuwasaidia wananchi kufanya shughuli za maendeleo na kujikwamua kiuchumi.
Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama akisoma maandishi ya uzinduzi wa jengo la masijala ya ardhi lililojengwa na MKURABITA katika Kijiji cha Maweni, Halmashauri ya Wilaya ya Meru mkoani Arusha mara baada ya kuzindua rasmi masijala hiyo wakati wa ziara yake ya kikazi iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za MKURABITA katika Halmashauri hiyo. Wanaoshuhudia ni Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongella pamoja na watendaji wengine wa Serikali.

“Kitendo cha MKURABITA kupima na kukabidhi hatimiliki za kimila, tayari imeshakuondolea umaskini, hivyo ni namna sasa ya wewe uliyenufaika na hatimiliki hiyo kufuata maelekezo ya kuitumia kwa maendeleo yako kwani hati hiyo ni dhamana yako ya kupata mkopo,” Mhe. Jenista amesisitiza

Mhe Jenista amewasisitiza wananchi hao kutoogopa kukopa fedha kwa ajili ya kufanya shughuli za maendeleo kwani mtu akitaka kuwa na maendeleo hawezi kuepuka kukopa.
Wananchi wa Kijiji cha Karangai na Maweni, Halmashauri ya Wilaya ya Meru mkoani Arusha wakimsikiliza Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama (hayupo pichani) alipokuwa akizungumza nao wakati wa ziara yake ya kikazi ya Waziri Jenista iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za MKURABITA katika Halmashauri hiyo.

“Msigope kukopa kwani mikopo ndiyo inayowasaidia wengi kuinuka kiuchumi na ndio maana Serikali imewarasimishia ardhi ili mpate hati ambazo zitawasaidia kukopa na kufanya shughuli za maendeleo ili lengo la serikali la kuona uchumi wa mtu mmoja mmoja unakua linafikiwa.,”Mhe. Jenista ameongeza.

Katika kuwawezesha wananchi hao kukopa, Mhe.Jenista ameziomba taasisi za kifedha kuitikia wito wa serikali wa kushusha riba hadi kufikia digitali moja.
Mkuu wa Mkoa wa Arusha, Mhe. John Mongella akitoa salamu za mkoa wake kabla ya kumkaribisha Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama kuzungumza na wananchi wa Kijiji cha Karangai na Maweni, Halmashauri ya Wilaya ya Meru wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista katika Halmashauri ya Meru iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za MKURABITA katika Halmashauri hiyo.

Aidha, Mhe. Jenista amewataka watumishi wa masijali za ardhi alizozizindua kutenda haki katika kuwahudumia wananchi.

“Mhe. Rais Samia Suluhu Hassan kupitia MKURABITA amewajengea ofisi nzuri hivyo mtumie ofisi hizo kuwahudumia wananchi kwa kutenda haki, utendaji wenu wa kazi uwe tofauti na wengine,” Mhe. Jenista amesisitiza na kuongeza kuwa shughuli zote zifanyike kwa uwazi ili kutoipa rushwa nafasi.

Kwa upande wake, Mratibu wa MKURABITA, Dkt. Seraphia Mgembe amewasisitiza wananchi wa vijiji hivyo kutumia masijala zilizozinduliwa kufanya shughuli za maendeleo.
Mratibu wa MKURABITA, Dkt. Seraphia Mgembe akiwasilisha taarifa ya utekelezaji wa majukumu MKURABITA kwa Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, Menejimenti ya Utumishi wa Umma na Utawala Bora, Mhe. Jenista Mhagama wakati wa ziara ya kikazi ya Mhe. Jenista iliyolenga kukagua utekelezaji wa shughuli za MKURABITA katika Halmashauri Wilaya ya Meru.

“Lengo la kujengwa kwa masijala hizi ni kufanya shughuli za maendeleo na sio vinginevyo, hivyo mzitumie vizuri ili kuhakikisha maendeleo ya mmoja mmoja na taifa kwa ujumla yanapatikana,” Dkt. Mgembe amesisitiza. 

Mhe. Jenista yuko mkoani Arusha kwa ziara ya kikazi ambapo pamoja na kuzindua masijala katika Vijiji vya Karangai na Meru katika Halmashauri ya Wilaya ya Meru, alizindua pia Kituo Jumuishi cha Urasimishaji na Uendelezaji wa Biashara na katika Halmashauri ya Wilaya ya Arusha.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news