SHIRIKA NYUMBA: UNADAIWA KALIPE!

NA LWAGA MWAMBANDE

NOVEMBA Mosi, mwaka huu Shirika la Nyumba la Taifa (NHC) limeanza kutekeleza kampeni kabambe ya miezi miwili ambayo inalenga kukusanya madeni kwa wapangaji wa nyumba zake waliopo na waliohama kote nchini.

Ni madeni ambayo yanakadiriwa kufikia zaidi ya shilingi bilioni 20. Fedha hizo ambazo ni mali za Watanzania zinatajwa iwapo zikilipwa mapema zitasaidia kuboresha na kuendeleza miradi mbalimbali ya nyumba nchini ili kuwezesha wananchi wengine kupata makazi.

Meneja Habari na Uhusiano wa NHC,Bw.Muungano Saguya hivi karibuni amewaeleza waandishi wa habari kuwa, kampeni hiyo itadumu hadi Desemba 30, mwaka huu na itaongozwa na kauli mbiu ya 'Lipa Kodi ya Nyumba kwa Maendeleo ya Taifa letu'.

Kila mmoja wetu anatambua juhudi mbalimbali zinazofanywa na shirika hilo za kuhakikisha linatekeleza miradi mingi ya nyumba kadri iwezekanavyo hapa nchini, ili wengi wetu tuweze kuishi katika nyumba hizo za gharama nafuu na zenye mahitaji yote ya msingi. Mshairi wa kisasa, Lwaga Mwambande anasema, dawa ya deni ni kulipa ili uishi kwa amani, endelea;


1.Unadaiwa kalipe,
Usichelewe kalipe,
Vipi wewe uwakope,
Shirika letu la Nyumba?

2.Toka Janwari kalipe,
Sikae bure kalipe,
Hatutaki uwakope,
Shirika letu la Nyumba.

3.Mepewa muda kalipe,
Kibali chao wakupe,
Vinginevyo yaja chepe,
Utolewe kwenye nyumba.

4.Miezi mbili kalipe,
Wala usikwepekwepe,
Huku malazi wakupe,
Shirika letu la Nyumba.

5.Umeshachoka walipe,
Ukishalipa usepe,
Hata Mungu muogope,
Hizo jua zetu nyumba.

6.Mefunguliwa utepe,
Wakaribishwa kalipe,
Keshi si barua pepe,
Shirika letu la Nyumba.

7.Nenda wewe kawalipe,
Wajenge nyumba watupe,
Nasi tukae tulipe,
Shirika letu la Nyumba.

8.Wanajenga wasikope,
Fedha unayo kalipe,
Wanakungoja kawape,
Shirika letu la Nyumba.

9.Usiishi kama kupe,
Nyumba zetu utukope,
Sifanye tukuogope,
Shirika letu la Nyumba.

10.Kopa kwingine ulipe,
Kwenye nyumba usisepe,
Hebu kusanya ulipe,
Shirika la nyumba.

11.Shirika la Nyumba wape,
Mnaotaka walipe,
Wasiishi kama kupe,
Kwenye hizo zenu nyumba.

12.Lakini wale mapepe,
Subirini wawalipe,
Kisha fukuza wasepe,
Waziache zenu nyumba.

13.Safisha ziwe nyeupe,
Na mazingira yalipe,
Kusibakie matope,
Zivutie kama nyuma.

14.Wakija wengine wape,
Wasomawaaa weupe,
Hakiki wasiwakope,
Tena msije kuyumba.

15.Dola gawio mtupe,
Miradi mipya ikope,
Maendeleo yalipe,
Nchi tuzidi kutamba.

Lwaga Mwambande (KiMPAB)
lwagha@gmail.com 0767223602

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news