Prof.Ole Gabriel asisitiza uboreshaji matumizi ya TEHAMA mahakamani

NA TIGANYA VICENT

MTENDAJI Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel amewataka maafisa wa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kuboresha matumizi ya teknolojia hiyo mahakamani ili kuwezesha uharakishaji wa utekelezaji wa jukumu la utoaji haki kwa wananchi.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel akitoa hotuba ya ufunguzi wa Mkutano wa Maafisa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano (TEHAMA) kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini Desemba 27, 2022 ambao unaofanyika katika ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

Prof.Ole Gabriel alitoa wito huo Desemba 27,2022 wakati akifungua mkutano wa Maafisa TEHAMA kutoka mikoa mbalimbali hapa nchini unaofanyika katika ukumbi wa Kituo Jumuishi cha Utoaji Haki (IJC) Dodoma.

“Mifumo ikikaa vizuri itasaidia kupunguza mapungufu yaliyojitokeza katika utendaji kwa mwaka uliopita. Naomba mboreshe mifumo yenu, tunahitaji kuona TEHAMA inapewa nafasi katika utendaji kazi za Mahakama wa kila siku,"alisema Mtendaji Mkuu huyo.

Aliwaeleza Maafisa hao kuwa uimarishaji wa matumizi ya TEHAMA mahakamani utachochea pia ongezeko wa ufanisi na tija katika utoaji wa haki kwa wananchi wengi kwa gharama nafuu.
Baadhi ya Maafisa Teknolojia ya Habari na Mawasiliano(TEHAMA) wa Mahakama ya Tanzania kutoka Mikoa mbalimbali wakifuatilia hotuba ya ufunguzi wa mkutano huo Desemba 27, 2022.

Prof Ole Gabriel alifafanua zaidi ya kuwa mkutano huo ni muhimu kwa watumishi hao kupata nafasi ya kubadilisha uzoefu wa baadhi ya mambo, hivyo ni heshima ya kipekee kwao kwa sababu Mahakama inakwenda kubadilika katika matumizi ya TEHAMA.

Alisema, msukumo walionao ni kuimarisha zaidi matumizi ya TEHAMA kwa ngazi zote za Mahakama ambapo hadi sasa asilimia 99 ya mashauri yanafunguliwa kwa njia ya mtandao ili kuwarahisishia wananchi upatikanaji wa huduma katika mazingira nafuu.
Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel(katikati) akiwa katika picha ya pamoja na Meza Kuu baada ya ufunguzi wa Mkutano huo. Wengine ni Naibu Msajili wa Mahakama Kuu Kanda ya Dodoma Mhe.Silvia Lushasi(kushoto) na kulia ni Mkurugenzi wa Kurugenzi ya TEHAMA(DICT) Mahakama ya Tanzania Bw.Enock Kalege. 

Aidha, Prof. Ole Gabriel alisema zaidi ya asilimia 70 ya mashauri yanatoka kwenye Mahakama za Mwanzo na kusema kuwa ni vema wakaweka nguvu katika kuimarisha matumizi ya TEHAMA katika Mahakama hizo ili wananchi wengi nao waweze kufikiwa na huduma hizo.

Wakati huo huo Mtendaji Mkuu huyo wa Mahakama ya Tanzania alisema hivi sasa wameanzisha huduma mbalimbali kwa ajili ya kuwawezesha wananchi kutoa maoni yao na kuuliza maswali pale wanapoona hawakutendewa haki ili wapate ufafanuzi sahihi kwa kutumia mifumo mbalimbali.
Meza Kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Maaafisa TEHAMA wanawake wa Mahakama ya Tanzania baada ya ufunguzi wa Mkutano huo.

Alitaja huduma zinazoendelea ni Kipindi cha Sema na Mahakama cha kila siku ya Jumanne kuanzia saa 12.30 jioni hadi saa 1.30 usiku kupitia Runinga ya ITV na kile cha Shirika la Utangazaji la Tanzania (TBC) cha siku ya Alhamisi kuanzia saa 12.00 jioini hadi saa 1.00 usiku.

Prof. Ole Gabriel aliongeza kuwa njia nyingine ambayo imeanzishwa na Mahakama ni kutoa maoni au kuuliza maswali kupitia Kituo cha Taarifa cha Mahakama ya Tanzania (Call Center) kwa namba 0752500400 au namba ya bila malipo ya 0800750247.

“Kadhalika tumefungua laini ya kushugulikia ndoa na mirathi pekee. Mikakati iliyopo ni kuboresha miundombinu ya TEHAMA na matumizi ya Mahakama mtandao hivyo tunakwenda kuwekeza zaidi kwenye eneo hili,” alisisitiza.
Meza Kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama ya Tanzania, Prof. Elisante Ole Gabriel(katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Maaafisa TEHAMA kutoka Makao Makuu ya Mahakama ya Tanzania baada ya ufunguzi wa Mkutano huo.

Prof. Ole Gabriel aliwaomba wananchi kutumia mifumo mbalimbali iliyoanziswa na Mahakama ya Tanzania kupata majawabu ya maswali na kero zao badala ya kusafiri na kutumia fedha nyingi kwa jambo ambalo suluhu yake wangeipata wakiwa nyumbani.

Aliongeza kuwa hivi sasa Mahakama ya Tanzania ipo kwenye hatua za mwisho za majaribio ya matumizi ya mfumo wa akili bandia ambao utakuwa ukitafsiri mambo mbalimbali na kuandika nakala za hukumu.

Prof. Ole Gabriel aliwataka Maafisa TEHAMA kubadilika na kufikiria nje ya boksi ili waweze kuendana na kasi ya utendaji wa Mahakama kupitia kiongozi wao ambaye ni Jaji Mkuu wa Tanzania Mhe. Prof. Ibrahim Hamis Juma.
Mkurugenzi wa TEHAMA (DICT) wa Mahakama ya Tanzania, Bw.Enock Kalege alitoa maelezo ya utangulizi kabla ya ufunguzi wa Mkutano huo.

Naye Mkurugenzi wa Kurugenzi ya TEHAMA(DICT), Bw. Enock Kalege akizungumza katika hafla hiyo alisema Maafisa hao wanakutano ili kutathimini utekelezaji wao wa Mpango Mkakati wa Mahakama ya Tanzania na kuboresha maeneo ambayo hawakufikia malengo. Alisema mkutano huo unajumuisha Maafisa TEHAMA 49 kutoka Mikoa yote ya Tanzania bara.
Meza Kuu ikiongozwa na Mtendaji Mkuu wa Mahakama Prof. Elisante Ole Gabriel (katikati waliokaa) ikiwa katika picha ya pamoja na Maaafisa TEHAMA kutoka Mahakama Kuu Divisheni mbalimbali baada ya ufunguzi wa mkutano wao.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news