Waziri Kairuki awataka Machifu kuhimiza jamii kulinda miradi ya maendeleo idumu

NA OR-TAMISEMI

WAZIRI wa Nchi, Ofisi ya Rais Tawala za Mikoa na Serikali za Mitaa (OR-TAMISEMI), Mhe. Angellah Kairuki amewataka machifu ambao ni viongozi wa kimila kuhamasisha jamii kulinda miundombinu ya miradi ya maendeleo.
Ametoa wito huo wakati akisimika machifu wa Kipare kwenye hafla iliyofanyika kwenye Kata ya Suji wilayani Same mkoani Kilimanjaro.

Mheshimiwa Kairuki amesema Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt.Samia Suluhu Hassan imeleta fedha nyingi za miradi ya maendeleo katika halmashauri zote nchini, hivyo jamii zina wajibu kushiriki kuilinda na kuitunza miradi hiyo ili iweze kudumu.
"Machifu ni watu muhimu na wana mchango mkubwa kwenye jamii zetu, hivyo niwasihi mtumie nafasi zenu kuhamasisha jamii yetu kutunza miundombinu ya miradi inayoletwa na Serikali katika maeneo yetu,"amesema.

Kairuki alitaja baadhi ya miradi mikubwa inayotekelezwa na Serikali kwa hivi sasa kuwa ni ujenzi wa madarasa 8,000 nchi nzima yanayogharimu shilingi bilioni 160.
"Kwa mwaka 2022/2023, Serikali imetoa fedha shilingi bilioni 160 kujenga madarasa 8,000 kwenye shule za sekondari ili kuwezesha wanafunzi wote wenye sifa ya kujiunga na kidato cha kwanza kwa mwaka 2023 wanaenda shule kwa wakati mmoja,"amesema.

Kairuki amesema pia kupitia Mradi wa Kuimarisha Elimu ya Sekondari (SEQUIP), Serikali itajenga shule za sekondari za kata 1,000 katika kipindi cha miaka mitano kuanzia 2021-2025.
"Kwa mwaka 2021/2022 jumla ya shilingi bilioni 143.47 zimetolewa kwa ajili ya kujenga shule za sekondari 232 na shule 10 za sekondari za wasichana za mikoa,"amesema.

Pia Mheshimiwa Kairuki amesema, kupitia Mradi wa Uimarishaji Elimu ya Awali na Msingi (BOOST), Serikali itatumia shilingi trilioni 1.15 katika kutekeleza mradi huo kwa miaka mitano kuanzia mwaka 2022/23 hadi 2026/27.
"Na kwa mwaka 2022/23 shilingi bilioni 250.9 zimepangwa kutumika ambapo zaidi ya madarasa 9,000 ya shule za awali na msingi yatajengwa.

"Kupitia mradi wa BOOST shule za msingi zingine zitabomolewa kutokana na kuwa chakavu sana, zingine zitakarabatiwa, zingine zitagawanywa na kujengwa mpya kwa kadiri wataalamu watakavyoshauri kutokana na uchakavu wa shule au idadi kubwa ya wanafunzi,"amesema.
Hata hivyo, katika hafla hiyo, Chifu Reubern Amani Mnyuku amesimikwa kuwa mwenyekiti wa machifu wa Wapare.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news