Prof.Muhongo aendesha harambee ujenzi wa miundombinu ya elimu, walimu Bwai Sekondari

NA FRESHA KINASA

MBUNGE wa Jimbo la Musoma Vijijini mkoani Mara, Mheshimiwa Prof.Sospeter Muhongo ameendesha harambee ya kuchangia ujenzi wa miundombini katika Shule ya Sekondari mpya ya Bwai iliyopo katika Kata ya Kiriba wilayani humo.
Shule hiyo mpya iitwayo Bwai Sekondari inajengwa na kijiji kimoja cha Bwai Kumsoma ambapo itapunguza mrundikano wa wanafunzi kwenye madarasa ya Kiriba Sekondari sambamba na kutatua matatizo ya umbali mrefu kwa wanafunzi wa kata hiyo kwenda masomoni Kiriba Sekondari.

Sekondari hii ilifunguliwa wiki iliyopita na hadi jana Januari 19, 2023 wanafunzi 125 kati ya 153 tayari wameanza masomo yao ya Kidato cha Kwanza (Form I) sawa na asilimia 77.85 wameanza masomo.
Harambee hiyo iliyoendeshwa na Prof. Sospeter Muhongo imefanyika Januari 19, 2023 na kuhudhuriwa na wananchi, viongozi wao wakiwemo madiwani wao wawili Mheshimiwa Hamis Saire na Flora Magwa na viongozi wa Chama Cha Mapinduzi akiwemo Mwenyekiti wa CCM, Wanyanja Kabati.

Harambee hiyo inalenga ukamilishaji wa vyumba vitatu vya madarasa. Kwa sasa, vyumba vilivyokamilika na vinatumika ni vitatu. Ujenzi wa choo kipya chenye matundu manne. Kwa sasa, ipo choo chenye matundu nane.
Pia ujenzi wa Jengo la Utawala ambalo msingi wake umekamilika. Kwa sasa, Ofisi ya Walimu ni chumba kimoja cha darasa.

Aidha, ujenzi ni endelevu, na michango ni endelevu hadi hapo miundombinu muhimu itakapokamilika, ikiwemo, maabara tatu za masomo ya sayansi, maktaba, nyumba za walimu, viwanja vya michezo.
Michango iliyopatikana katika harambee hiyo ni saruji mifuko 51, misumari kilo tatu, fedha taslimu shilingi 610,000 pia nguvu kazi wataendelea kujitolea kujenga bila malipo.

Mbunge wa jimbo, Mheshimiwa Prof.Sospeter Muhongo amechangia saruji mifuko 100, mabati bando mbili (mabati 24).
"Harambee ya walimu wa kujitolea Bwai Sekondari ina jumla ya walimu watano, akiwemo Mkuu wa Shule, Sekondari hii haina walimu wa masomo ya English, Mathematics na Physics,"imeeleza taarifa iliyotolewa na Ofisi ya Mbunge na kuongeza kuwa.

"Wanakijiji wakiwemo wazazi wa wanafunzi wanaosoma hapo, wameamua kuajiri walimu wa kujitolea kwa posho ya shilingi 200,000 kwa kila mwalimu kwa mwezi. Wazazi watachangia Shilingi elfu 3,000 kila mwezi."imeeleza taarifa hiyo.

Aidha, Mbunge wa jimbo, Prof. Muhongo atachagia shilingi 100,000 kwa kila mwalimu kwa mwezi, yaani jumla ya shilingi 300,000 (laki tatu) kila mwezi kwa walimu watatu.
Pia kuhusu vitabu vya Maktaba. Mbunge wa Jimbo Prof. Muhongo ametoa boksi nne za vitabu vya Maktaba kwa Sekondari hiyo mpya yenye kidato kimoja.
Picha za juu zinaonesha matukio mbalimbali ya jana kwenye shule mpya (Bwai Sekondari) ya Kijijini Bwai Kumsoma, Kata ya Kiriba.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news