Serikali ya Awamu ya Sita itaendelea kugharamia utekelezaji miradi ya kimkakati-Dkt.Mpango

NA MWANDISHI WETU

MAKAMU wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango amesema Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Mheshimiwa Dkt. Samia Suluhu Hassan, itaendelea kugharamia utekelezaji wa miradi ya kimkakati ili kuhakikisha inakamilika na kuchangia katika ukuaji wa uchumi wa wa taifa.
Makamu wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango akisikiliza maelezo kutoka kwa Mkurugenzi Mkuu wa Shirika la Reli Tanzania (TRC), Masanja Kadogosa wakati akielezea kuhusu ujenzi wa Reli ya Kisasa (SGR) Kipande cha nne Tabora – Isaka yenye urefu wa Kilometa 165 wakati wa hafla ya Uwekaji Jiwe la Msingi la Ujenzi wa Reli hiyo iliofanyika Isaka Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga leo Januari 18, 2023.

Makamu wa Rais amesema hayo wakati wa hafla ya uwekaji jiwe la msingi Ujenzi wa wa Reli ya Kisasa (SGR) Kipande cha nne Tabora-Isaka yenye urefu wa Kilometa 165 inayogharimu shilingi Trilioni 2.09 hafla iliofanyika eneo la Isaka Wilaya ya Kahama mkoani Shinyanga leo tarehe 18 Januari 2023.

Amesema jitihada hizo zimeendelea kuleta matokeo chanya ikiwemo kuongezeka kwa mchango wa sekta ya ujenzi na usafirishaji katika pato la taifa kwa mwaka kufikia wastani wa asilimia 23 katika kipindi cha 2020 – 2021 ukilinganisha na wastani wa asilimia 21.7 katika kipindi cha 2018-2019.
Makamu wa Rais ameitaka Wizara ya Ujenzi na Uchukuzi, Bodi ya Wakurugenzi na Wafanyakazi wa TRC kuendelea kutimiza wajibu wao wa kusimamia vizuri utekelezaji wa miradi ya kimkakati ili iweze kukamilika kwa wakati na ubora unaotakiwa.

Aidha amewasihi kuongeza uzalendo, kujituma na ubunifu pamoja na kufanya kazi kibiashara na kwa kuzingatia Sheria, Kanuni na taratibu wakati wa utekelezaji wa miradi hiyo.

Halikadhalika Makamu wa Rais ametoa wito kwa mkandarasi wa reli ya kisasa kipande cha nne Tabora – Isaka kuhakikisha vijana wa mkoani Shinyanga na Tabora wanapewa kipaumbele katika fursa mbalimbali za ajira zinazoweza kutolewa kwa kundi hilo.

Pia kuwapa fursa wakinamama kwa upande wa utoaji wa huduma mbalimbali kama za chakula ili mradi huo uweze kuchochea shughuli za kiuchumi katika mkoa huo na mikoa jirani.
Vilevile Makamu wa Rais ameagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuwatafuta na kuwachukulia hatua kali za kisheria wote wanaohujumu ujenzi wa mradi wa reli ya kisasa kwa wizi wa vifaa mbalimbali vya ujenzi ikiwemo mafuta.

Aidha ameagiza kubainishwa kwa mtandao mzima wa wahujumu hao hususani wanunuzi wa mali za wizi kutoka katika mradi wa SGR ili wakamatwe na kuchukuliwa hatua kali za kisheria.

Makamu wa Rais amesema ushiriki wa Tanzania katika mtangamano wa Eneo Huru la Biashara la Afrika, umeendelea kuufungua uchumi wa taifa kwa kushiriki katika soko la watu takribani bilioni 1.4.

Ameongeza kwamba Serikali ya Awamu ya Sita imeweka kipaumbele kwenye ujenzi wa miradi ya kimkakati ambayo itaweka mazingira mazuri ya kuchochea ukuaji endelevu wa kiuchumi wa nchi.

Aidha ameeleza kwamba tayari serikali imefanya uwekezaji mkubwa kwenye Reli, Bandari, Barabara, Mkongo wa Taifa, Shirika la Ndege, meli, kwenye maziwa pamoja na vivuko.

Kwa upande wake Waziri wa Ujenzi na Uchukuzi Prof. Makame Mbarawa amesema mara baada ya kukamilika kwa uwekezaji unaofanyika katika ujenzi wa miradi ya kimkakati, sekta hiyo itatoa mchango mkubwa kwa taifa moja kwa moja pamoja na kusaidia kukua kwa sekta zingine.

Prof Mbarawa amesema uwekezaji unaofanyika una manufaa makubwa kwa watanzania na wananchi wa Afrika mashariki kwa ujumla.

Ameongeza kwamba mradi wa reli ya kisasa utachochea kuimarika zaidi kwa Bandari ikiwemo bandari ya dar es salaam inayotumiwa ziaidi na nchi majirani pamoja na kupunguza kwa kiasi kikubwa muda wa usafirishaji wa mizigo.

Awali akitoa taarifa za Ujenzi wa Mradi huo Mkurugenzi wa Shirika la Reli Tanzania Masanja Kadogosa amesema uwezo wa kubeba mizigo kupitia reli ya kisasa utakua ni tani 120 kwa behewa ikiwa ni mara tatu ya reli ya sasa yenye uwezo wa kubeba tani 40 kwa behewa.

Aidha amesema kupitia ujenzi huo,TRC inatarajia kuboresha chuo cha reli kilichopo Tabora na kuweza kutoa shahada ya uandisi katika reli mara baada ya kukamilika.

Vilevile amesema TRC imeendelea kuokoa gharama kwa kiasi kikubwa kupitia mikataba ya ujenzi wa reli ambayo hairuhusu ongezeko la gharama kutoka kwa mkandarasi kutokana na mabadiliko ya bei za vifaa na malighafi.

Pia Kadogosa amesema uwekezaji katika mradi huo umeleta tija katika uchumi wa wananchi wazawa ikiwemo viwanda kupata fursa ya kutoa huduma za ugavi na malighafi za ujenzi ikiwemo nondo na saruji.

Amesema jumla ya ajira elfu ishirini zimetolewa kwa wananchi wa Tanzania kupitia ujenzi wa reli ya kisasa na zabuni 1476 zimetolewa zenye thamani ya shilingi trilioni 1.8.
Ameongeza kwamba TRC wataaendelea kusimamia kutimiza malengo ya serikali ya kuhakikisha ujenzi wa miundombinu ya reli unatekelezwa kwa viwango na thamani ya fedha ya fedha inaonekana.

Mradi wa Ujenzi wa wa Reli ya Kisasa (SGR) Kipande cha nne Tabora – Isaka yenye urefu wa Kilometa 165 unatarajia kukamilika machi 2026.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news