Waziri Bashe akiri matumizi ya mbolea Mkoa wa Rukwa yameongezeka

NA MWANDISHI WETU

WAZIRI wa Kilimo, Hussein Bashe ameeleza kuwa, matumizi ya mbolea kwa Mkoa wa Rukwa msimu huu wa kilimo (2022/2023) yameongezeka tofauti na msimu wa kilimo 2021/2022.
Amesema, matumizi ya mbolea kwa Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi kwa msimu wa kilimo 2021 ilikuwa ni tani 1,600 lakini msimu wa kilimo 2022/2023 kuanzia tarehe 15 Agosti, 2022 mpaka tarehe 3 Januari 2023 kiasi cha tani 842 sawa na asilimia 50 ya mbolea zilizotumika msimu uliopita wa kilimo kimetumika.
Viongozi wa taasisi zilizo chini ya Wizara ya Kilimo wakifuatilia maelekezo ya Waziri wa Kilimo, Hussein Bashe wakati wa mkutano wa kuhitimisha ziara yake mkoani Rukwa tarehe 4 Januari, 2023 katika ukumbi wa mikutano wa mkoa huo. Kulia ni Mkurugenzi Mtendaji wa Mamlaka ya Udhibiti wa Mbolea Tanzania (TFRA), Dkt. Stephan Ngailo.

Ameeleza kuwa, matumizi ya mbolea kwa msimu uliipita yanalingana na matumizi ya mbolea kwa nusu msimu wa mwaka 2022/23 japo msimu wa kilimo bado unaendelea na kubainisha muitikio wa matumizi ya mbolea umekuwa mkubwa kutokana na bei za mbolea kushuka pamoja na kupanda kwa bei ya nafaka kulikowafanya wakulima kuongeza ukubwa wa mashamba yao ya kulima.
Waziri Bashe amebainisha hayo tarehe 4 Januari, 2023 alipokuwa katika kikao cha majumuisho ya ziara yake ya siku mbili mkoani Rukwa kilichohuhusisha watendaji wa Serikali na Chama Wafanyabiashara wa mbolea, waingizaji na wasambazaji wa mbolea pamoja na wananchi.

Akitoa taarifa ya mauzo ya kiasi cha mbolea kilichouzwa kwa msimu uliopita wa kilimo, Waziri Bashe amesema, msimu wa 2021 waliuza Tani 1120 na mpaka tarehe 3 Januari 2023 wameuza kiasi cha tani 4000 kwa kampuni la OCP wakati ETG kwa msimu wa 2021 waliuza tani 1700 mpaka tarehe 03 Januari, 2023 kiasi cha tani 1700 za mbolea zimeuzwa.
"Ningekuta kiasi cha mbolea kilichofika Nkasi ni kidogo kuliko msimu uliopita ningejua kuna crisis lakini kwa hali ilivyo bado tupo katika nafasi nzuri na uzuri usambazaji wa mbolea unaendelea," Waziri Bashe alisisitiza.

Amesema, katika kutatua changamoto ya upatikanaji wa mbolea karibu na maeneo ya wakulima Mamlaka ya Serikali ya Mkoa wa Rukwa itateua vituo vitakavyosajiliwa ili kuwawezesha mawakala kufikisha mbolea katika maeneo hayo kwani mbolea haiwezi kuuzwa katika vituo ambavyo havijasajiliwa.
Ameongeza kuwa, wamekubaliana na makampuni kuhakikisha wanapeleka mbolea karibu na wakulima na kubainisha atawafutia leseni endapo hawatafuata maelekezo aliyoyatoa wakati wa ziara hiyo.
Aidha, ameishukuru kampuni ya usambazaji wa mbolea la ETG kwa kuitika wito baada ya maelekezo aliyotoa ambapo tayari wamepeleka na kuanza kuuza mbolea katika Halmashauri ya Wilaya ya Nkasi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news