Miaka 180 jela kwa makosa mawili ya unyang'anyi huko Sengerema

NA DIRAMAKINI

MAHAKAMA ya Wilaya ya Sengerema Mkoa wa Mwanza imewahukumu watu sita kila mmoja kifungo cha miaka 30 (wote jumla miaka 180) kwenda jela kwa makosa mawili ya unyang'anyi wa kutumia silaha katika kesi namba 67 na 68 zote za mwaka huu.

Akisoma mashitaka yanayowakabili mbele ya Hakimu mkazi Mwandamizi wa Mahakama ya Wilaya Sengerema, Evodi Kisoka, mwendesha mashtaka wa Serikali Mkaguzi wa Polisi (Insp) Martha Chacha aliwataja kwa majina washitakiwa hao kuwa ni Salum James, (28) mkazi wa Katoro mkoani Geita,

Abel Samwel, (18) mkazi wa Katoro Mkoani Geita, Juma John, (30) mkazi wa Kijiji cha Buzilasoga, Deus Magili, (25) mkazi wa Katoro Mkoani Geita, Razaro James, (23) mkazi wa Katoro Mkoani Geita, na Medrick Lisolanya (37) mkazi wa Busilasoga wilayani Sengerema.

Martha aliiambia mahakama kuwa, washitakiwa hao walitenda makosa mawili ya unyang'anyi wa kutumia silaha kinyume na kifungu namba 287 A cha sheria na kanuni ya adhabu sura 16 toleo la mwaka 2022 kwa wakati tofauti.

Washitakiwa hao waliyetenda makosa hayo mnamo Machi 29, mwaka huu majira ya saa 9:20 na 08:00 usiku huko katika Kijiji cha Buzilasoga wilayani Sengerema mkoani humo ambapo majira ya saa 09:20 wote kwa pamoja waliiba TV nchi 17 aina ya Sundar, simu mbili aina ya Tecno, betri moja ya sola, flashi moja mali zote hizo zikiwa ni za Halima Daudi mkazi wa Buzilasoga wilayani humo.

Kosa la pili ni unyang'anyi wa kutumia silaha kinyume na kifungu namba 287 A cha sheria na kanuni ya adhabu sura ya 16 toleo la mwaka 2022, kuwa mnamo Machi 29, 2023 muda wa saa 08:00 usiku huko katika Kijiji cha Buzilasoga wilayani humo washitakiwa wote kwa pamoja waliiba TV nchi 17 aina ya Abodar, simu moja aina ya Itel na pesa taslimu shilingi 100,000 ikiwa ni mali ya Bonifas Bugota mkazi wa Buzilasoga.

Hata hivyo, washitakiwa wote kwa pamoja walikiri kutenda makosa hayo hivyo Mahakama imewatia hatiani kwa kuwafunga jela miaka 30 kila mmoja ili iwe fundisho kwa watu wengine.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news