TanTrade na UCSAF kutoa huduma ya intaneti Maonesho ya Sabasaba

NA DIRAMAKINI

MAMLAKA ya Maendeleo ya Biashara Tanzania (TanTrade) pamoja na Taasisi ya Mfuko wa Mawasiliano kwa Wote (UCSAF) zimekutana na kufanya kikao cha jinsi ya kutoa huduma ya mawasiliano ya intaneti (Wireless Internet) kwenye Uwanja wa Maonesho wa Mwalimu J.K Nyerere ndani ya Halmashauri ya Manispaa ya Temeke jijini Dar es Salaam.
Huduma hiyo itatolewa kwa kipindi chote cha Maonesho ya 47 ya Kimataifa ya Biashara Dar es Salaam (Maonesho ya SabaSaba) yatakayofanyika kuanzia Juni 28 hadi Julai 13, 2023. 

Kikao hicho kimefanyika Juni 8, 2023 katika Ofisi za TanTrade jijini Dar es Salaaam kwa lengo la kuboresha na kurahisisha miundombinu ya mawasiliano ili kuwasaidia washiriki pamoja na watembeleaji kuweza kupata mawasiliano kwa njia rahisi na haraka zaidi katika kipindi chote cha maonesho hayo.
Akizungumza katika kikao hicho, Bw. Fortunatus Mhambe, Kaimu Mkurugenzi wa Ukuzaji Biashara, TanTrade kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, Bi. Latifa M. Khamis ameishukuru Taasisi ya UCSAF kwa kutoa huduma hiyo inayolenga kurahisisha mawasiliano na kuboresha maonesho yawe na mvuto zaidi.
"Kwa niaba ya Mkurugenzi Mkuu, natoa shukrani zangu za dhati kwa Taasisi ya UCSAF kwa kukubali kuboresha huduma za internet katika kipindi cha maonesho, hivyo tunapenda kuuhabarisha umma kwamba katika maonesho hayo, huduma za intaneti zitakuwa zimeimarishwa na kuboreshwa kwa ajili ya watembeleaji na waoneshaji na kuwarahisishia kuonesha biashara zao kwa njia rahisi zaidi,"amesema.
Naye Mratibu kutoka UCSAF Kanda ya Pwani, Bw. Baraka Elieza amesema kuwa,Taasisi ya UCSAF itahakikisha kuwa huduma za intaneti zinakuwa nzuri na zenye kuleta tija katika Uwanja wa Maonesho na kuwafanya waoneshaji pamoja watembeleaji kuweza kufurahia huduma hizo kuanzia Juni 28 hadi Julai 13, 2023.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news