Waziri Mhandisi Masauni aanika mafanikio ya Jeshi la Polisi chini ya uongozi wa Rais Samia

NA GODFREY NNKO

WAZIRI wa Mambo ya Ndani ya Nchi, Mheshimiwa Mhandisi Hamad Masauni amesema,chini ya uongozi wa Serikali ya Awamu ya Sita inayoongozwa na Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan, Jeshi la Polisi kupitia wizara hiyo limepiga hatua kubwa.

Miongoni mwa mafanikio ambayo jeshi hilo limefanikiwa ni kuhakikisha linaimarisha ulinzi na usalama wa raia nchini kote.

Mheshimiwa Waziri Mhandisi Masauni ameyasema hayo jioni ya Juni 4, 2023 kupitia mjadala uliondaliwa na Msemaji Mkuu wa Serikali ukiangazia jitihada za kuimarisha usalama wa raia na mali zao na kuboresha Jeshi la Polisi nchini Tanzania.

Aidha, mjadala huo ambao ulirushwa moja kwa moja kupitia Clubhouse mbali na kuwaleta pamoja maafisa mbalimbali wa wizara, Jeshi la Polisi pia wananchi walipata fursa ya kuchangia mjadala huo na kuuliza maswali.

Mafanikio

Waziri Mhandisi Masauni amesema, "Niseme tu kama kuna fanikio moja kubwa sana ambalo tunaweza kujivunia katika kipindi hiki cha Serikali ya Awamu ya Sita ni kuimarika kwa hali ya usalama nchini.

"Na hii inadhihirika wazi, kipindi hiki tulikumbana na changamoto nyingi sana, na ninyi ni mashaidi miongoni mwake ni changamoto za uhalifu, lakini jambo la faraja ni kwamba hakuna hata jaribio moja la uvunjifu wa amani katika nchi hii ambalo Jeshi la Polisi lilishindwa kulidhibiti kwa kiwango kikubwa, na ndiyo maana nchi yetu imeendelea kuwa na amani na usalama wa hali ya juu.

"Na kimsingi ndiyo jukumu la Jeshi letu la Polisi,lakini kubwa zaidi ni maboresho ambayo kutokana na maelekezo na miongozo ya Amiri Jeshi Mkuu, ninyi ni mashaidi Mheshimiwa Rais alivyoingia amedhamiria kuleta mabadiliko katika jeshi letu la polisi na amefanya hivyo.

"Kwa kuchukua hatua kadhaa, moja katika hatua muhimu sana ni kuunda Tume ya Haki Jinai ambayo tunatarajia itakuja na mapendekezo makubwa ambayo yanaweza kuleta mabadiliko makubwa katika Jeshi letu la Polisi.

"Lakini mbali na hayo kumekuwa na ongezeko kubwa sana la kibajeti, fedha ambayo imeongezeka katika kipindi kifupi cha Serikali ya Mheshimiwa Mama Samia Suluhu Hassan ni ya kuridhisha, tulikuwa tunazungumzia bajeti ya shilingi bilioni 604 kwa mwaka 2021/22 mpaka kuja bilioni 734 kwa mwaka 2022/23 ambapo tunazungumzia ni ongezeko la asilimia zaidi ya 21, na ongezeko hili limekwenda kugusa maeneo muhimu.

"Moja katika maeneo ambayo tunajivunia sana ambayo yalikuwa ni changamoto na ilikuwa ikiwaathiri wananchi kwa kiasi fulani, wakati mwingine mwananchi anaweza kuwa na shida, kwenye ngazi za wilaya, za kata anaweza kwenda polisi akaambiwa gari aina mafuta.

"Lakini Mheshimiwa Rais ameelekeza ongezeko la bajeti,moja katika ya mambo ambayo imekwenda kugusa ni kuhakikisha kwamba fedha ya mafuta ya kuhudumia magari ya polisi kwa ajili ya kuhudumia ngazi mpaka za chini, zinakwenda moja kwa moja, na hiyo imesaidia kuimarisha huduma za wananchi katika kuweza kupata huduma kwenye Jeshi lao la Polisi.

"Lakini vile vile tulikuwa na changamoto ya askari wetu wamekuwa wakistaafu,hatukuweza kupata ajira za askari wapya hivyo kufanya askari wachache waliopo kubeba mzigo wa askari wengine.

"Lakini, Mheshimiwa Rais tangu ameingia madarakani, katika muda mfupi tumepata ajira za askari wasiopungua 7000 mpaka 8000 mpaka tunavyozungumza sasa hivi wapo askari wanaendelea na mafunzo yao kwenye Chuo cha Polisi.

"Na hivyo basi inasaidia kupunguza upungufu wa askari katika jeshi letu, lakini hata eneo la upandishwaji vyeo, zaidi ya askari 29,020 wamepandishwa vyeo, na leo hii tunazungumzia mafanikio ya kulishusha Jeshi la Polisi kwa wananchi.

"Jukumu la msingi la usalama linaanzia kwa mwananchi mwenyewe, lakini hatuwezi kufanya hivyo, kama jeshi halijawa karibu nao, na kupitia huu utaratibu wa kupandisha vyeo, tumeweza kupandisha vyeo askari wa nyota moja ambao takribani wote ni wahitimu na wamepelekwa kwenye kata nchi nzima,"amefafanua kwa kina Mheshimiwa Waziri Mhandisi Masauni.

Mazingira bora

Ameendelea kufafanua kuwa, "kama hiyo haitoshi tumeweza kuandaa utaratibu wa mazingira mazuri ya kufanya kazi kwao, nimezungumzia mafuta, lakini pamoja na usafiri katika bajeti iliyopita imetengwa takribani bilioni 15 ambapo hadi tunapozungumza sasa hivi takribani magari 101, pikipiki 336 sehemu yake zipo njiani, niseme kwa sababu tayari tumeshaanza mchakato wa manunuzi.

"Sema pikipiki hizo zitakwenda moja kwa moja kwenye kata na magari yale yanakewenda katika kila wilaya ya nchi hii, tumeshapeleka tayari magari 150 mengine katika maeneo mbalimbali ambayo yalikuwa na mapungufu, lakini lengo kubwa ni kuhakikisha tunatekeleza maelekezo ya Amiri Jeshi Mkuu kuhakikisha kila wilaya ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania ina gari mpya kwa ajili ya kuhudumia wananchi na kila kata ambapo kuna askari kata kuhakikisha kuna pikipiki ya kuhudumia wananchi.

"Hivi karibuni tumekuja na mpango wa maboresho kupitia Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Polisi kwa kufanya maboresho ya matumizi kuhakikisha mfuko huo asilimia 60 pamoja na miradi mingine ambayo tunatarajia kupitia maboresho hayo yanakwenda katika mpango kabambe wa kuhakikisha ujenzi wa vituo vya polisi nchi nzima.

"Kwa hiyo hii sasa ni dhana na dhamira ya Jeshi la Polisi ya kuhakikisha linakuwa karibu zaidi na wananchi ambapo kule ndiko kuna changamoto nyingi za kiusalama na matukio mengi ya uhalifu yanaanzia huko.

"Tunaweza kufanya kwa ufanisi mkubwa, mafanikio mengine ni mafunzo kwa askari, kuboresha mazingira yao ya kazi na utendaji kazi, moja katika jambo muhimu sana ni kuhakikisha kwamba askari wetu wanafanya kazi kisasa,

"Na ndiyo maana kupitia mwaka huu wa fedha kama mtakumbuka bajeti ambayo nimeiwasilisha hivi karibuni, nilizungumzia miradi kadhaa ambayo tunakwenda kuianzisha ama kuikamilisha katika mwaka huu wa fedha inayolenga kuhakikisha kwamba tunaliimarisha Jeshi letu la Polisi, kwa maana ya vifaa, zana,mbinu na weledi wa kufanya kazi.

"Nikiachilia mbali vitendea kazi kama magari, nimesema tutanunua boti 10 mwaka huu wa fedha, lakini halikadhalika na vifaa mbalimbali, lakini tunakwenda kuhakikisha tunakuwa na Jeshi la Polisi ambalo linatumia mifumo ya kisasa,

"Moja katika jambo kubwa sana ambalo tunatarajia tuanze nalo ni kwamba tuna utaratibu wa kuwa na miji salama, tukianzia katika mikoa mikubwa mitatu ukiwemo Dar es Salaam, mkoa wa kibiashara, Mkoa wa Arusha, mkoa wa kitalii na makao makuu ya nchi Dodoma kwa kuanzia katika mwaka huu wa fedha.

"Eneo lingine ni kuhakikisha katika usalama barabarani kuna maboresho makubwa sana ambayo yanaendelea, kwa ujumla mafanikio ni mengi sana,"amesisitiza Waziri Mhandisi Masauni.

Dhumuni

Mheshimiwa Waziri Mhandisi Masauni awali alifafanua kuwa, Jeshi la Polisi nchini lina majukumu mbalimbali, "Jeshi la Polisi, madhumuni yake nimeeleza kuwa ni kulinda usalama wa raia na mali zao,lakini yakiwa yanajikita katika kutimiza lengo hilo,ili kuifanya nchi yetu kuendelea kubaki salama, na amani iweze kutengamaa katika nchi yetu.

"Na hiyo inaweza kufikiwa kwa kutekeleza sheria mbalimbali ambazo tumezitunga ambazo zinaliwezesha Jeshi letu la Polisi kutekeleza majukumu yake ya kubaini, kuzuia uhalifu,kuwakamata, kuwahifadhi, kuwafikisha mahakamani, kukusanya, kuchunguza,kutoa ushaidi mahakamani, yote haya yanafanyika katika lengo hilo hilo moja la kuhakikisha kwamba nchi yetu inaendelea kubakia katika hali ya amani na utulivu,"amesema Waziri Mhandisi Masauni.

Kamisheni mbalimbali

Mbali na hayo, Mheshimiwa Waziri Mhandisi Masauni amesema, Jeshi la Polisi nchini linatekeleza majukumu yake hayo kupitia kamisheni mbalimbali.

"Kwanza,kuna Kamisheni ya Upelelezi wa Makosa ya Jinai ambayo inahusu kufanya upelelezi wa makosa makubwa na madogo ya jinai, usalama barabarani pamoja na kutunza vielelezo na kupeleka mbele ya mahakama kwa ajili ya ushaidi, kutanzua pamoja na kupambana na uhalifu."

Pili, amesema ni Kamisheni ya Ushirikishwaji wa Jamii ambapo inafanya kazi kubwa ya kulipeleka Jeshi la Polisi kwa jamii katika kushirikiana nayo hususani kupitia utoaji wa elimu jinsi ya kushiriki katika kudumisha ulinzi, ushiriki wa madawati ya kijinsia na watoto.

Sambamba na utaribu wa vikundi mbalimbali vya ulinzi shirikishi kuanzia ngazi za vitongoji hadi juu, kusimamia mifumo na kutatua changamoto za kiulinzi na usalama katika kila kata, shehia, na kuanzisha Polisi Kata na Sheia.

Tatu, Mheshimiwa Waziri Mhandisi Masauni amesema ni Kamisheni ya Fedha na Logistiki ambayo inawajibika katika kueweka mipango ya Jeshi la Polisi ikiwemo kuandaa bajeti kila mwaka, kusimamia matumizi ya rasilimali fedha, mambo yanayohusu vifaa vya Jeshi la Polisi, upatikanaji wa ardhi, ujenzi wa ofisi na makazi ya askari, "Ingawa kupitia hili kuna maboresho mbalimbali tumefanya kupitia Shirika la Uzalishaji Mali la Jeshi la Polisi."

Nne, pia amesema wana Kamisheni ya Rasilimali Watu, hii inasimamia utendaji kazi, nidhamu ya askari pamoja na watumishi rai wote wa jeshi, kusimamia mifumo ya rasilimali watu.

Waziri Mhandisi Masauni amesema, kamisheni hiyo pia inawajibika kusimamia masuala ya ajira, maslahi, stahiki mbalimbali za askari, upandishwaji vyeo, pamoja na mambo mengine ikiwemo kupanga safu ya uongozi wa makamanda katika ngazi mbalimbali za mikoa na wilaya.

Tano, amesema ni Kamisheni ya Operesheni na Mafunzo ambayo inaratibu na kusimamia mafunzo mbalimbali ndani na nje ya nchi, kusimamia operesheni mbalimbali, kufanya doria, misako mbalimbali kwenye maeneo yote ya nchi yetu kuanzia baharini, kwenye maziwa, anga, nchi kavu, kuratibu na kusimamia ulinzi wa rasilimali mbalimbali za nchi.

"Kwa mfano madaraja, tuna miradi ya kimkakati ambayo Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt.Samia Suluhu Hassan ameisimamia kwa kasi ya kweli kweli, na maeneo hasa yanayohusu usalama barabarani. Sina maana ya kuchanganya hii na Kitengo cha Usalama Barabarani, lakini inapokuja operesheni huwa hatutofautishi."

Sita, amesema ni Kamisheni ya Uchunguzi wa Kisayansi, "hii ni kamisheni nyingine muhimu sana, ambayo hii inafanya uchunguzi wa matukio mbalimbali, wa kumbukumbu mbalimbali zilizohifadhiwa kwenye mabara,kwa lengo la kupata taarifa mbalimbali na vielelezo ikiwemo sampuli kwa ajili ya kuandaliwa kama ushaidi kwenye Mahakama."

Saba, Waziri Mhandisi Masauni amesema ni Kamisheni Mahususi ya Zanzibar, "ambayo yenyewe ina vitengo vinafanana na hivi ambavyo nimevizungumza, lakini inafanya shughuli, zile za kipolisi zote kwa upande wa Zanzibar zikiwemo operesheni kwa ujumla kuhakikisha amani na utulivu unaendelea kuwepo kwa upande wa Zanzibar, ikiwemo kwenye Sekta ya Utalii ambayo ni sekta muhimu kwa upande wa Zanzibar.

"Pamoja na mapambano dhidi ya changamoto za uhalifu zilizokuwa zimeongezeka katika kipindi cha karibuni kwa upande wa Zanzibar hususani masuala ya ubakaji, udhalilishaji na dawa za kulevya,"amefafanua Waziri Mhandisi Masauni.

Nane, amesema ni Kamisheni ya Intelijensia ya Jinai ambayo inawajibika kufanya ufuatiliaji na kukusanya taarifa zote za kiintelijensia zenye viashiria vya uhalifu wa jinai pamoja na kutoa taarifa za uhalifu huo kwa ajili ya kuwezesha kupatikana ama kuwakamata wahalifu hao au kudhibiti uhalifu. "Kwa hiyo huo ndiyo muundo wa Jeshi letu la Polisi, kwa ujumla wake."

Kuhusu wizara

Mheshimiwa Waziri Mhandisi Masauni akiielezea wizara yake kwa kifupi amesema kuwa, "Naomba nichukue fursa hii kutoa ufafanuzi kwa ufupi kabisa kuhusiana na Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa ujumla,Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi kwa ujumla ina vyombo ambavyo inasimamia, idara, taasisi na sekretarieti zisizopungua 18.

"Lakini kwanza inayochukua sehemu kubwa ni Jeshi la Polisi, na Jeshi la Polisi majukumu yake makubwa ni kulinda usalama wa raia na mali zao.

"Kwa sababu leo mada inahusu zaidi kuhusu Jeshi la Polisi nitakuwa na nafasi ya kuzungumzia kwa mapana zaidi kuhusu majukumu ya Jeshi la Polisi, mafanikio, changamoto, mikakati na hatua ambazo tunaendelea nazo katika kufikia malengo hayo ya kulinda usalama wa raia na mali zao kama mada inavyojieleza.

"Lakini, vile vile kuna Jeshi la Magereza, Jeshi la Magereza lenyewe lina majukumu makubwa ya msingi ya kutunza aina zote za wafungwa pamoja na kuwarekebisha tabia ili wale wafungwa watakaporejea uraiani wawe wema zaidi.
"Lakini, pia kuna Idara ya Uhamiaji, ambayo ina jukumu la kuthibitisha, kuwezesha uingiaji, ukaaji pamoja na utokaji wa raia na wageni nje ya nchi, kwa hiyo hayo ndiyo majukumu ya msingi ya Jeshi la Uhamiaji.

"Pia, tuna chombo kingine cha nne ambacho kinatambulika kama Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, na lenyewe hili malengo yake makubwa ya msingi ya kisheria ni kuokoa maisha ya watu na mali zao,katika majanga mbalimbali pamoja na kuzima moto kwa ujumla.

"Baada ya hapo, pia tuna Idara ya Wakimbizi, ambayo hii ina jukumu la kuwapokea na kuwahifadhi wakimbizi wanaoingia nchini pamoja na kuwatafutia suluhisho la kudumu wakimbizi hao, kama ni kuwarudisha makwao baada ya hali ya usalama kutengamaa katika maeneo yao au kuwapeleka katika nchi ya tatu.

"Lakini, vile vile kama wamejitokeza wakimbizi ambao wameendelea kubakia hapa nchini, wengine kupata uraia. Lakini, pia tuna Idara ya Huduma za Uangalizi, hii inaratibu na kusimamia uangalizi wa utekelezaji wa adhabu mbadala, kupitia zile sheria mbili, Kuna Sheria ya Huduma ya Jamii, pamoja na ile ya utaratibu wa vifungo vya nje, idara hii ndiyo mahususi kuratibu mambo hayo.

"Pia, tuna Ofisi ya Msajili wa Jumuiya, hii kazi yake ni kusajili taasisi za kidini na zisizo za kidini, pamoja na kuhakiki na kufuatilia utekelezaji wa majukumu yake kama yanakwenda sambamba na katiba zao.

"Lakini, pia tuna Idara ya Malalamiko, ambayo inahifadhi kumbukumbu za malalamiko, inapokea, inasikiliza, inachambua inayapatia ufumbuzi pamoja na kupelekea mrejesho kwa mlalamikaji, iwe malalamiko hayo yamelengwa katika moja ya vyombo vyetu ama katika wizara ama katika taasisi zilizo nje ya wizara.

"Lakini, pia tuna Sekretarieti ya Kupambana na Usafirishaji Haramu wa Binadamu, ambayo jukumu lake la msingi ni kuratibu na kwa kushirikiana na idara nyingine za Serikali na zisizo za Serikali kushughulikia kuzuia pamojan na kupambana na usafirishaji haramu wa binadamu.

"Pia, tuna Mamlaka ya Vitambulisho vya Taifa (NIDA), yenyewe ina jukumu la kusajili na kutambua raia pamoja na wakaazi wote ambao wanaishi nchini, wenye umri wa kuanzia miaka 18 na zaidi pamoja na kutoa vitambulisho vya Taifa kwa raia, wageni na wakimbizi ambao wanaishi nchini kihalali.

"Halikadhalika, tuna Tume ya Utumishi ya Jeshi la Polisi, Jeshi la Magereza, Jeshi la Zimamoto na Uokoaji, Jeshi la Uhamiaji ambalo lina mambo mengi, lakini moja wapo ni kumshauri Mheshimiwa Rais kuhusu mamlaka yake ya kikatiba yanayohusu uteuzi wa maafisa wa nafasi mbalimbali zilizo wazi katika vyombo vyetu.

"Lakini pia kutekeleza kwa kukasimiwa madaraka hayo na Mheshimiwa Rais kwa shughuli mbalimbali ambazo zinahihusu tume, yako mkasuala ambayo yanahusu upandishwaji vyeo, yako masuala yanayohusu nidhamu kwa askari na wakati mwingine masuala ambayo yanahusu rufaa zinazohusiana na vyombo hivyo vinne.

"Kwa hiyo hivyo ni miongoni mwa vyombo, ama taasisi aua idara zilizopo chini ya Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi, kuna idara nyingine kadhaa,lakini hizi ni idara ambazo zimekuwa zikitoa msaada kwa utekelezaji wa majukumu ya wizara ya moja kwa moja, kwa mfano kuna Idara ya Sheria, Idara ya Ununuzi,Ugavi na Fedha, Mawasiliano Serikalini na mengineyo, lakini cha msingi taasisi au idara ambazo zinagusa moja kwa moja wananchi ndiyo hizo ambazo nimeziorodhesha,"amefafanua kwa kina Mheshimiwa Waziri Mhandisi Masauni kupitia mjadala huo.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news