Mhandisi Saidy ataka kila mtumishi REA kuwajibika kikamilifu

DODOMA-Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy amesisitiza uwajibikaji kwa kila mtumishi wa Wakala ili kutekeleza jukumu lake kuu la kuhakikisha wananchi waishio vijijini wanatumia nishati bora kama zinazotumika mijini.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy akizungumza na wafanyakazi wa Wakala katika kikao kazi kilichofanyika Septemba 11, 2023 Dodoma.

Alikuwa akizungumza katika kikao kazi cha wafanyakazi wa REA kilichofanyika Septemba 11, 2023 jijini Dodoma kujadili masuala mbalimbali yanayolenga kuboresha utendaji kazi.

“Kila mmoja wetu anapaswa kuwa na utashi, kuweka jitihada na maarifa ili matunda ya kazi yetu yaonekane kwa wananchi,” amesisitiza.
Mkurugenzi Mkuu wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA), Mhandisi Hassan Saidy akizungumza na wafanyakazi wa Wakala (hawapo pichani) katika kikao kazi kilichofanyika Septemba 11, 2023 Dodoma. 

Kushoto ni Kaimu Mkurugenzi wa Utawala na Rasilimaliwatu, Adrophine Tutuba na kulia ni Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya (TUGHE), Tawi la REA, Swalehe Kibwana.

Akieleza zaidi, Mhandisi Saidy amesema wafanyakazi wa REA wanapaswa kuhakikisha utendaji kazi wao unaakisi dhamira ya Serikali ya kuwapatia fursa wananchi waishio vijijini kutumia nishati bora sawa na wale wanaoishi mijini.
Amesema kuwa, miradi mbalimbali inayotekelezwa na Wakala inaendelea vizuri na akawataka wafanyakazi kuendelea na moyo wa utendaji kazi kwa bidii ili miradi mipya iliyoanza kutekelezwa ikamilike kwa ufanisi.
Wafanyakazi wa Wakala wa Nishati Vijijini (REA) wakimsikiliza Mkurugenzi Mkuu wa REA, Mhandisi Hassan Saidy (hayupo pichani) wakati wa kikao kazi kilichofanyika Septemba 11, 2023 Dodoma.

Kwa upande wake, Mwenyekiti wa Chama cha Wafanyakazi wa Serikali na Afya (TUGHE), Tawi la REA, Swalehe Kibwana aliushukuru Uongozi wa Wakala kwa kujenga utaratibu wa kuzungumza na wafanyakazi ili kuwapatia fursa ya kueleza changamoto ikiwa zipo na kutoa maoni yao kuhusu masuala mbalimbali ya kazi.

Katika kikao hicho, wafanyakazi mbalimbali walitoa maoni kuhusu maeneo ya utendaji kazi yanayopaswa kuboreshwa na ni kwa namna gani.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news