TAWA yakabidhiwa rasmi mashamba ya wanyamapori Lente, Loldebes na Amani Arusha

NA BEATUS MAGANJA

SERIKALI ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania tarehe 3 Oktoba, 2023 imekabidhi rasmi mashamba ya Wanyamapori ya Lente, Loldebes na Amani yaliyopo Wilaya ya Monduli mkoani Arusha kutoka kwa Msajili wa Hazina na kwenda kwa Mamlaka ya Usimamizi wa Wanyamapori Tanzania (TAWA) kwa ajili ya shughuli za uhifadhi na uendelezaji wa utalii.
Mkuu wa Wilaya ya Monduli, Mhe. Joshua Nassari ambaye alikuwa mgeni rasmi katika hafla ya makabidhiano ya mashamba hayo iliyofanyika ndani ya eneo la mashamba maarufu "Makuyuni Wildlife Park" amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan kwa maamuzi yake ya kubadilisha matumizi ya mashamba kutoka kwenye shughuli za kilimo na kurasimisha ili yaweze kutumika kwa shughuli za uhifadhi na uendelezaji wa utalii.

Mhe. Nassari amesema, maamuzi hayo yanakwenda kufungua fursa nyingi zenye tija kwa wakazi wa Monduli kutokana na uwekezaji utakaofanywa na TAWA katika eneo hilo na kuitaka TAWA iliendeleze eneo hilo kwa haraka kwa kuwa ni eneo muhimu, lenye rasilimali nyingi na linafikika kirahisi.
Mkuu huyo wa Wilaya ameipongeza TAWA kwa juhudi inazozifanya katika kuboresha utendaji wa taasisi.

"Niwapongeze sana TAWA kwa "efforts" (juhudi ) ambazo mmezifanya tumeona mageuzi makubwa mno kwenye taasisi yenu kwa miaka ya hivi karibuni, tunaamini kwamba Ile "pace" mnayokwenda nayo na huku kwetu tunaamini kufikia mwakani mapato yetu ya Halmashauri yatakuwa yanaongezeka,"amesema.
Mwenyekiti wa Bodi ya Wakurugenzi ya TAWA, Meja Jenerali mstaafu Hamis Semfuko amemshukuru Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Amiri Jeshi Mkuu, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan Kwa kuridhia TAWA ikabidhiwe mashamba hayo kwa ajili ya Uhifadhi na uendelezaji wa utalii
Aidha, Semfuko amesema kwakuwa eneo hilo lina fursa kubwa ya Utalii TAWA imelipa jina la kibiashara la *"Makuyuni Wildlife Park"* na kwamba maono ya Bodi ya Wakurugenzi ya TAWA ni kuongeza mapato na kuimarisha Uhifadhi na italitumia eneo hilo kwa utalii wa picha na kwa kuanza itajenga miundombinu wezeshi ili kuwezesha shughuli za uhifadhi na Utalii kufanyika kikamilifu pamoja na kuvutia wawekezaji
Kwa upande wake Kamishna wa Uhifadhi wa TAWA, Mabula Misungwi Nyanda amesema, kutokana na imani kubwa ya Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwa TAWA hata kuikabidhi mashamba hayo, TAWA italipa imani hiyo kwa kuwa wabunifu katika kuongeza mapato katika eneo hilo, ikizingatiwa kuwa eneo hilo awali lilitumika kama mashamba ya kilimo lakini kutokana na umuhimu wake kiuhifadhi Serikali imeamua litumike kwa shughuli za kiuhifadhi.
Pia, amewaomba wananchi wanaozunguka eneo hilo kuendelea kushirikiana na TAWA katika ulinzi wa rasilimali zilizopo na kuhakikisha zinanufaisha jamii kupitia shughuli za Utalii

Awali akielezea historia ya mashamba hayo, Mkurugenzi wa ubinafsishaji, ufuatiliaji na tathmini-Ofisi ya Msajili wa Hazina, Mohamed Nyasama amesema mnamo tarehe 02 Juni, 2022 Msajili wa Hazina kupitia barua yake alikabidhi mashamba hayo kwa TAWA kwa ajili ya usimamizi wa muda wakati wakisubiri maelekezo ya Mamlaka.
Ameongeza kuwa, tarehe 27 Februari 2023 mamlaka ilitoa maamuzi na kupitia barua ambayo iliandikwa kwa Katibu Mkuu Wizara ya Fedha ilitoa maelekezo kuhusiana na matumizi ya eneo hilo na kupitia barua ya Katibu Mkuu Kiongozi walitaarifiwa kuwa mamlaka imeridhia mapendekezo ya kamati kuwa mashamba ya steyn (yaan shamba la Lente, Loldebes na Amani) yakabidhiwe rasmi kwa TAWA ili yatumike kwa ajili ya uhifadhi na uendelezaji wa utalii.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news