Serikali yaridhishwa na uwekezaji katika Kiwanda cha Sukari TPC

KILIMANJARO-Serikali ya Awamu ya Sita chini ya Rais Samia Suluhu Hassan imeeleza kuridhishwa na uwekezaji wake katika Kiwanda cha Sukari TPC kilichoko mkoani Kilimanjaro.

Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu(kulia) akijadiliana jambo na Afisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Sukari cha TPC, Marius Jacobs, (kushoto) mara baada ya mkutano mkuu wa wanahisa uliofanyika mkoani Kilimanjaro.

Akizungumza kwa niaba ya Serikali akiwa mkoani Kilimanjaro leo Novemba 16, 2023, Msajili wa Hazina, Nehemia Mchechu, alisema wao kama wawekezaji wamefurahishwa na kuridhishwa na ufanisi katika uendeshaji wa kiwanda hicho.

Alisema, ufanisi huo unatokana na faida iliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2022/23 ambapo kiwanda hicho kilipata faida baada ya kodi ya Shs. bilioni 72.7 kutoka katika mauzo ya Shs. bilioni 235, huku gawio kwa wanahisa likiwa Shs. bilioni 69.9.

“Sisi wawekezaji tumefurahi na kuridhishwa na ufanisi katika uendeshaji wa kiwanda hiki cha sukari cha TPC Limited, ufanisi huu unatokana na faida iliyopatikana katika kipindi cha mwaka 2022/23 ambapo kiwanda kimeweza kuzalisha faida baada ya kodi ya shilingi 72.7. bilioni kutoka katika mauzo ya shilingi bilion 235 huku gawio kwa wanahisa ikiwa ni shilingi bilioni 69.9, alisema Mchechu baada ya kikao cha wanahisa kilichofanyika mkoani Kilimanjaro.

Mchechu anasema, tangu mwaka 2000 kiwanda hicho kimekuwa kikiongeza uzalishaji mwaka hadi mwaka ambapo kwa sasa uzalishaji wa sukari umeongezeka kutoka Tani 36,000 za mwaka 2000 hadi kufikia Tani 116,700 kwa mwaka 2022/23.

Katika kiwanda hicho cha TPC Limited, Serikali inamiliki asilimia 25 ya hisa wakati kampuni ya Sukari Investment Limited inamiliki asilimia 75 baada ya ubinafsishaji uliofnyika mwaka 2000.

Anaeleza kwamba, ongezeko hilo la uzalishaji wa sukari limetokana na ongezeko la mavuno ya miwa ambapo kwa mwaka huu kiwanda kimevuna miwa zaidi ya Tani 1,150,000.

Katika uzalishaji wa sukari kwa mwaka huu, TPC Limited imezalisha zaidi ya tani 116,700 katika kipindi cha Juni 2022 hadi Machi 2023, hiki ni kiwango kikubwa sana cha sukari ambacho hakijawahi kuzalishwa katika miaka yote tangu TPC Limited kuanza uzalishaji wake mwaka 1936,” anasema.

Anasema, wakati wanafanya ubinafsishaji wa kiwanda hicho, serikali ilikuwa imeweka malengo shamba la TPC baada ya kuwa imeongezewa eneo la shamba la Kahe, itaweza kuzalisha tani 750,000 kwa mwaka, lakini kwa sasa wanazalisha Tani 1,150,000 ambayo ni juu ya malengo waliyokuwa wamewekewa na serikali wakati wa ubinafsishaji.

Eneo lile lile lakini uzalishaji unazidi kuwa mkubwa kutokana na tija katika uzalishaji kwani kwa mwaka huu TPC tumeweza kutoa tija ya wastani wa tani 148 (tani mia moja na arobaini na nane) kwa hekta, kiwango ambacho ni cha juu barani Afrika, na ni moja kati ya viwango bora vitatu duniani,” anasisitiza Mchechu.

Akizungumzia sababu ya ufanisi na mafanikio hayo, Mchechu anasema, Serikali ya Awamu ya Sita imeweka nguvu na jitihada kubwa za kuhamasisha kilimo na kuvutia uwekezaji katika kilimo hususani katika sekta ya sukari na hilo limeweza kufungua fursa nyingi kwenye sekta ya sukari nchini.

Anasema, mambo ambayo yamefanyika katika kipindi cha Serikali ya Awamu ya Sita ni pamoja na kuendelea kulinda soko la ndani dhidi ya sukari inayoingizwa yenye kiwango cha chini na kuja kushindana na sukari inayozalishwa nchini yenye kiwango bora.

Anaeleza kuwa, kitendo hicho kimefanya sukari kuendelea kuuzwa katika bei nzuri na hivyo kuhamasisha wazalishaji kuendelea kuwekeza zaidi katika soko la sukari.

Tumeshuhudia serikali imekuwa na mfumo unaoeleweka na endelevu wa uagizaji wa sukari kutoka nje ya nchi na hii ni kutokana na maboresho yaliyofanyika katika Sheria ya Sukari pamoja na Kanuni zake ambapo uagizaji wa sukari kutoka nje ya nchi umewekewa utaratibu mzuri zaidi, anasema.

Anasema, eneo lingine ambalo serikali imefanya ni kuhamasisha na kuwahakikishia wawekezaji mazingira mazuri ya uwekezaji, hali ambayo imechangia kupanda kwa idadi ya wawekezaji kutoka ndani na nje ya nchi wanaowekeza katika sekta ya sukari.

Vipo viwanda mbavyo vimeanza kufanya kazi lakini pia kuna viwanda vingine vinakuja kuweza kuongeza uzalishaji wa sukari nchini, hivyo katika mazingira haya tumeona Serikali ya Awamu ya Sita imesukuma mbele jitihada za kukuza kilimo hususan cha miwa, ili kuongeza uzalishaji wa sukari hapa nchini,” anasisitiza.

Mchechu anabainisha pia kwamba, katika kuunga mkono jitihada hizo za serikali, TPC kwa mwaka huu wanatazamia kuwekeza fedha Dola 45 milioni hadi 50 milioni kwa kujenga kiwanda kipya cha kuchakata Molasses ambayo imekuwa ikibaki baada ya uzalishaji wa sukari.

Bodi yetu leo itaidhinisha matumizi ya fedha zaidi ya Dola 45 milioni ama Dola 50 milioni kwa ajili ya kuweka kiwanda kingine cha uchakataji Molasses na kuweza kuzalisha bidhaa nyingine ambayo itakuwa ni spirit kwa ajili ya matumizi ya viwanda na watumiaji wengine,” akaongeza.

Anasema, kiwanda hicho kitajengwa TPC na ujenzi wake unatarajiwa kuanza mapema mwaka 2024, na kwamba hicho ni kiwango kikubwa cha fedha kitakachowekezwa ambapo ni pamoja na kukuza zao la miwa na bidhaa zinazotokana na zao la miwa.

Anaeleza kuwa, uwekezaji huo kwa TPC utakuza ajira pamoja na kuongeza mapato ya ndani ya kiwanda na kuwezesha kulipa kodi nyingi zaidi na manufaa mengine yatakayopatikana kutokana na uwekezaji huo.

Mchechu anaongeza kuwa, jambo kubwa zaidi kutakuwa na ongezeko la uzalishaji wa nishati ya umeme ambapo katika kiwanda hicho wanatarajia kufunga mashine nyingine ya kuzalisha umeme na hivyo kutakuwa na ziada ya 4MW hadi 7MW ambazo zitaingizwa katika Gridi ya Taifa.

Msajili wa Hazina, Nehemiah Mchechu(katikati) , Afisa Mtendaji Mkuu wa Kiwanda cha Sukari cha TPC, Marius Jacobs, (kulia) pamoja na Afisa Mtendaji Utawala wa TPC, Jaffari Ally wakifuatilia kwa umakini maswali ya waandishi wa habari (hawapo pichani) katika mkutano na vyombo vya habari baada ya mkutano mkuu wa wanahisa uliofanyika mkoani Kilimanjaro.

Akizungumzia mchango wa Kiwanda cha Sukari cha TPC kwa serikali, Jafarry Ally, ambaye ni Mkuu wa Utawala katika kiwanda hicho, anasema TPC imeweza kulipa kodi, ushuru pamoja na gawio kwa serikali zaidi ya Shs. bilioni 99, kiwango ambacho ni kikubwa ukilinganisha na kiwango cha Shs. bilioni 2 kilichokuwa kikitolewa wakati kampuni hiyo imebinafsishwa mwaka 2000.

Anasema, sababu kubwa ya kuongezeka kwa kiwango hicho ni uzalishaji,mauzo mazuri na ulipaji sahihi wa kodi kwa mujibu wa sheria na miongozo ya ulipaji kodi.

Mwaka 2010 ndipo kiwanda kilianza kulipa gawio serikali na hadi mwaka 2022/2023 tumekuwa tukilipa gawio na kiwango kimekuwa kikiongezeka mwaka hadi mwaka na kuifanya TPC kuongoza kwa miaka mitatu mfululizo kwa kutoa gawio zuri na kubwa serikalini kuliko mashirika mengine yote ambayo serikali ina hisa kidogo,” anasema.

Akizungumzia mchango wa kiwanda hicho kwa jamii, Ally anasema, kwa kupitia shirika lao lisilo la kiserikali la FTK, wamekuwa wakitumia Shs. bilioni 1.2 kwa mwaka kwa ajili ya kuhudumia jamii ya vijiji vinavyowazunguka ambapo fedha hiyo inaelekezwa kwenye miradi mbalimbali ya maendeleo katika sekta za elimu, afya, miundombinu na miradi endelevu ya vijiji kama miradi ya umwagiliaji.

Kwa upande wa utoaji wa huduma katika vijiji vinavyotuzunguka, tumeendelea kuboresha huduma na kwa upande wa elimu, hivi karibuni tumejenga shule ya sekondari ya Chekereni/Weruweru (CHEWE) ambayo ni ya serikali, na serikali ilituletea fedha za Uviko-19 ikaja kuongezea majengo ambayo imefanya shule hiyo kuwa na vitu vingi vilivyokamilika.

Ni shule inayoanza lakini ina vitu vyote muhimu ikiwemo madarasa, vyoo, jiko, madawati, maabara zote pamoja na jengo la utawala na shule hii itazinduliwa hivi karibuni baada ya serikali kukamilisha uwekaji wa samani.

Lakini pia tumeweza kutoa huduma za afya na kujenga mundombinu ya barabara kutokana na uwezo tunaokuwa nao ikiwa ni pamoja na kuchimba visima na kujenga mabwawa ya kuoshea mifugo katika vijiji vinavyotuzunguka,” anasema Ally.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news