Tuna orodha ya wasanii wote wanaojihusisha na dawa za kulevya, ni suala la muda tu-Kamishna Jenerali Lyimo

NA GODFREY NNKO

MAMLAKA ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) imesema kuwa, ina orodha ya wasanii wote wanaojihusisha na matumizi ya dawa za kulevya ikiwemo kutumia vipawa vyao kuhamasisha matumizi ya dawa hizo ambazo ni haramu nchini.
Hayo yamesemwa Novemba 14, 2023 jijini Dar es Salaam na Kamishna Jenerali wa mamlaka hiyo, Aretas Lyimo wakati akifunga semina ya siku mbili iliyoandaliwa na DCEA kwa wahariri wa vyombo vya habari nchini ili kuwajengea uwelewa.

"Lakini, pia tunayo orodha ya wale watu wanaohamasisha matumizi ya dawa za kulevya, na wasanii ambao ndiyo wanaongoza katika uhamasishaji wa dawa za kulevya na tuna orodha ya wasanii wanaotumia dawa za kulevya.

"Na hii orodha tutaitumia, na tunayo sheria pia, ambayo ukiangalia kwenye Sheria yetu Kifungu cha 17 na 18 kinatupa mamlaka ya kumkamata mtu yeyote tunayemhisi anatumia dawa za kulevya.

"Tunamkamata, tunamchukua na tunampima, tuna maabara ya kisasa tunajenga sasa hivi. Itakamilika muda wowote na vifaa tulishaagiza, kwa sasa vimeshafika bandarini, ile maabara ni kwa ajili ya kutekeleza hii sheria.

"Wale wote tunaowahisi wanatumia dawa za kulevya na hapo hapo wanaendelea kuhamasisha watu watumie dawa za kulevya, tunawakamata kupitia Sheria Namba 17 na 18 tunaenda tunawapima, sheria inaturuhusu na tukishawapima, tukabaini kwamba wanatumia dawa za kulevya tunawapeleka mahakamani.

"Tukishawapeleka mahakamani, hukumu yao ni kifungo cha miaka mitatu gerezani. Wakishafungwa ile miaka mitatu, endapo hakimu au vipimo vitathibitisha kwamba yeye tayari ameshakuwa mraibu wa zile dawa, hakimu atatoa hukumu pengine kabla hajatekeleza ile adhabu apelekwe kwenye kituo cha kupata tiba.

"Kwenye kifungu Namba 31 cha sheria yetu, kinaruhusu kwamba, mtu akishahukumiwa kwa amri ya hakimu pamoja na kifungo alichohukumiwa kule gerezani, lakini anatakiwa apate tiba.

"Kwa hiyo, Kifungu Namba 31 kinaturuhusu tuanze kumtibu yule mtu. Kwa hiyo, nitoe wito kwa wale wasanii wote wanaotumia dawa za kulevya na ambao tayari orodha yao tunayo wako wasanii wanaotumia Cocaine tunayo orodha yao, wako wasanii wanaotumia Heroin tunayo orodha yao.

"Lakini, pia wako wasanii wanaotumia bangi na orodha yao tunayo, kwa hiyo wale wote tunawapa muda wa kujirekebisha.

"Hii mitambo yetu ikikamilika tutaweza kushughulika nao wote, kwa sababu wale ndiyo wanaohamasisha jamii katika matumizi ya dawa za kulevya kwa nyimbo zao, kwa mavazi wanayovaa mengine yanakuwa na majani ya bangi.

"Lakini, pia kwa maneno yao na matendo yao ambayo yanaonesha dhairi kwamba wanatumia dawa za kulevya. Kwa nini, sasa hivi hatufanyi hivyo wakati sheria inaturuhusu? Ni kwa sababu tulikuwa hatujakamilisha ujenzi wa maabara yetu.

"Kwa hiyo,maabara ikikamilika tutaanza kushughulika na wale wote, yaani mtu akihamasisha tu matumizi ya dawa za kulevya tunamkamata, halafu tunaenda kumpima tukikuta anatumia dawa za kulevya tunampeleka mahakamani sheria inaruhusu.

"Akishahukumiwa miaka mitatu na kama vipimo vikathibitisha amekuwa mraibu anaanza kupata huduma ya dawa ili kuondoka kwenye ule uraibu, hilo tutalifanya.

"Kwa hiyo, waandishi wa habari, wahariri wafikishieni taarifa wasanii kwamba tunawapa muda, maabara hii ikishakamilika tutaanza kushughulika nao na BASATA (Baraza la Sanaa Tanzania) tulishafanya nao kikao kuhusiana na wasanii wale wanaohamasisha dawa za kulevya.

"Na tayari waliridhia, tulikutana na Katibu Mtendaji na waliridhia tutapeleka ile orodha tutaanza kuwaita na kama watakaidi, sheria ipo tunwapa wito wa pili, atakayekaidi anafungiwa kufanya kazi za usanii hapa nchini.

"Kwa hiyo, tutahakikisha hatutajali ukubwa wa msanii, hatutajali anapendwa kiasi gani na wananchi, lakini ilimradi anahamasisha dawa za kulevya, ilimradi anatumia dawa za kulevya vipimo ni vya kisasa vitaonesha.

"Tutachukua hatua, kwa hiyo tuwaombe wasanii ni kioo cha jamii, wasanii ndiyo wanatakiwa wapeleke ujumbe mzuri kwa wananchi sasa wao matokeo yake, baadhi yao wanaanza kutumia dawa za kulevya, lakini wengine wanashawishiwa na wasanii wenzao katika matumizi ya dawa za kulevya.

"Lakini, pia nitoe wito kwa wale wananchi wote ambao kwa nafasi zao zozote walizo nazo wanatumia dawa za kulevya na kuhamasisha dawa za kulevya, niwaombe waache.

"Na kuanzia sasa hivi, wale wote watakaokuwa wanaendelea kuhamasisha matumizi ya dawa za kulevya ikiwemo kwa mavazi, kwa maneno, kwa kutumia majukwaa yao pia tutachukuwa hatua ikiwa ni pamoja na kuwapima ili kuhakikisha kama na wao wanatumia dawa za kulevya tuweze kubaini, na tukikuta wanatumia tunachukua hatua za kisheria.

"Ni hii Sheria yetu Namba 17 na 18 ambapo tukiwakuta na uraibu kulingana na Sheria Namba 31 tutaanza kuwapa tiba, kwa hiyo tunawaomba muwafikishie ujumbe, kwamba tutaanza kuchukua hatua kuanzia sasa hivi,kwa wale wanaotumia na kuhamasisha dawa za kulevya,"amefafanua kwa kina Kamishna Jenerali wa DCEA, Aretas Lyimo.

Kuhusu DCEA

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) ilianzishwa chini ya kifungu cha 3 cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 ya Mwaka 2015. Sheria hii iliifuta Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya. Kuanzishwa kwa Mamlaka Kulitokana na mapungufu yaliyokuwepo katika mfumo wa udhibiti wa dawa za kulevya.

Mapungufu hayo yalikuwa ni pamoja na Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya iliyoanzishwa na Sheria ya ya Kuzuia Biashara Haramu ya Dawa za Kulevya Namba 9 ya mwaka 1995 kukosa nguvu ya kisheria ya kupeleleza, kufanya uchunguzi na kukamata wahalifu wa dawa za kulevya.

Kutokana na mapungufu hayo, Baraza la Mawaziri katika kikao chake cha tarehe 8 Novemba, 2007 (Waraka Na 60/2007) liliagiza, kurekebisha au kufuta Sheria ya Kuzuia Biashara Haramu ya Dawa za Kulevya Namba 9 ya mwaka 1995, ili kukidhi matakwa na changamoto za udhibiti wa matumizi na biashara ya dawa za kulevya.

Baraza la Mawaziri liliagiza kuundwa kwa chombo cha kupambana na dawa za kulevya chenye uwezo kiutendaji kwa kukipa mamlaka ya ukamataji, upekuzi na upelelezi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola ili kuongeza ufanisi wa udhibiti wa dawa za kulevya nchini.

Kufuatia agizo hilo, tarehe 24/03/2015 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilitunga na kupitisha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 ya Mwaka 2015 na kuanza kutumika rasmi tarehe 15 Septemba, 2015 kupitia tangazo la Serikali namba 407 (GN NO.407/2015).

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ilianza kutekeleza majukumu yake kikamilifu tarehe 17 Februari, 2017 baada Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kumteua Kamishna Jenerali.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news