Kamishna Jenerali Lyimo:Mtu akitumia dawa za kulevya anapotea kiroho, kimwili na kijamii pia

NA GODREY NNKO

KAMISHNA Jenerali wa Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya nchini (DCEA), Aretas Lyimo amesema, kazi ya kupambana na dawa za kulevya imejikita kuokoa roho za watu, hivyo jamii iendelee kushirikiana na mamlaka kufichua watu wanaojihusisha na biashara hiyo haramu nchini.

Ameyasema hayo Novemba 14, 2023 jijini Dar es Salaam wakati akifunga semina ya siku mbili kwa wahariri wa vyombo vya habari nchini ambayo iliandaliwa na mamlaka hiyo kuwajengea uelewa.

"Kazi tunayoifanya (DCEA) kuhakikisha tunafikisha ujumbe na elimu kwa jamii ni sawa na wale wainjilishaji, lakini ni sawa na anaposimama Shehe kwenye mimbari kuhubiria watu wasitende dhambi.
 
"Ni sawa na anaposimama Mchungaji pale kwenye mimbari kuhakikisha kwamba anawahubiria watu wamrudie Mungu.

"Ndicho hiki hiki tunachokifanya, kwa hiyo, kazi tunayoifanya ni sawa na kazi wanayoifanya wale watumishi wa Mungu kwa sababu hapa tunaokoa roho za watu, kwa sababu mtu akishatumia dawa za kulevya anapotea kiroho, kimwili na kijamii pia.

"Kwa hiyo, sasa tunachokifanya ni kuwaokoa kuwarudisha ili Taifa lisiendelee kuingia kwenye matumizi ya dawa za kulevya,"amefaanua Kamishna Jenerali Lyimo.

Mbali na hayo, Kamishna Jenerali Lyimo amewaomba wahariri wa vyombo vya habari nchini na wanahabari kuendelea kutumia kikamilifu kalamu zao ili kusaidia kutoa elimu kwa jamii kuhusu madhara ya dawa za kulevya ambayo yamekuwa chanzo cha watu wengi kushindwa kutimiza malengo yao.

Amesema, Taifa linahitaji nguvu kazi kubwa ya watu wenye nguvu ya kufanya kazi kwa bidii na utimamu wa akili ili waweze kushiriki katika shughuli za maendeleo kwa ustawi bora wa jamii zao na Taifa lenyewe.


Kuhusu DCEA

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya (DCEA) ilianzishwa chini ya kifungu cha 3 cha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 ya Mwaka 2015. Sheria hii iliifuta Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya. Kuanzishwa kwa Mamlaka Kulitokana na mapungufu yaliyokuwepo katika mfumo wa udhibiti wa dawa za kulevya.

Mapungufu hayo yalikuwa ni pamoja na Tume ya Kuratibu Udhibiti wa Dawa za Kulevya iliyoanzishwa na Sheria ya ya Kuzuia Biashara Haramu ya Dawa za Kulevya Namba 9 ya mwaka 1995 kukosa nguvu ya kisheria ya kupeleleza, kufanya uchunguzi na kukamata wahalifu wa dawa za kulevya.

Kutokana na mapungufu hayo, Baraza la Mawaziri katika kikao chake cha tarehe 8 Novemba, 2007 (Waraka Na 60/2007) liliagiza, kurekebisha au kufuta Sheria ya Kuzuia Biashara Haramu ya Dawa za Kulevya Namba 9 ya mwaka 1995, ili kukidhi matakwa na changamoto za udhibiti wa matumizi na biashara ya dawa za kulevya.

Baraza la Mawaziri liliagiza kuundwa kwa chombo cha kupambana na dawa za kulevya chenye uwezo kiutendaji kwa kukipa mamlaka ya ukamataji, upekuzi na upelelezi kwa kushirikiana na vyombo vingine vya dola ili kuongeza ufanisi wa udhibiti wa dawa za kulevya nchini.

Kufuatia agizo hilo, tarehe 24/03/2015 Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania lilitunga na kupitisha Sheria ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya Na. 5 ya Mwaka 2015 na kuanza kutumika rasmi tarehe 15 Septemba, 2015 kupitia tangazo la Serikali namba 407 (GN NO.407/2015).

Mamlaka ya Kudhibiti na Kupambana na Dawa za Kulevya ilianza kutekeleza majukumu yake kikamilifu tarehe 17 Februari, 2017 baada Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kumteua Kamishna Jenerali.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news