Tumieni Mpimbwe Fm kutangaza mazao-Mheshimiwa Pinda

NA MUNIR SHEMWETA

MBUNGE wa Jimbo la Kavuu na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Mheshimiwa Geophrey Pinda amewataka wanawake wa Mpimbwe katika Wilaya ya Mlele Mkoa wa Katavi kukitumia Kituo cha Redio Jamii cha Mpimbwe Fm kutangaza mazao wanayozalisha ili waweze kupata masoko.

Mheshimiwa Pinda ametoa kauli hiyo tarehe 26 Februari 2024 katika Kata ya Usenya alipozungumza na wanawake wa kata hiyo wakati wa sherehe za kuelekea siku ya wanawake duniani inayoadhimishwa kila mwaka mwezi machi.
Mbunge wa Jimbo la Kavuu na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Mheshimiwa Geophrey Pinda akizungumza na wanawake katika Kata ya Usenya Halmashauri ya Mpimbwe tarehe 26 Februari 2024 wakati wa sherehe za kuelekea siku ya wanawake duniani inayoadhimishwa kila mwaka mwezi Machi.

Wanawake katika Halmashari ya Mpimbwe wamejiwekea utaratibu katika kuelekea Siku ya Wanawake Duniani wakutane kata kwa kata kwa lengo la kusheherekea na kujadili changamoto zinazowakabili katika maeneo yao.

‘’Redio ile ni ya kwetu na wala siyo ya mtu binafsi na ndiyo maana imejengwa pale Halmashauri ya Mpimbwe tutaitumia kujitangaza, tunazalisha mazao mengi kama mpunga, mahindi ili wanunuzi watufuate,’’ alisema Mheshimiwa Pinda.

Kwa mujibu wa Mbunge huyo wa Jimbo la Kavuu, wanawake wa Mpimbwe wakiitumia vizuri redio hiyo hasa katika kutangaza mazao yao basi ana uhakika wa bei ya mazao kupanda kwani kwa sasa wanaowabana wanajiona wako peke yao.
Sehemu ya wanawake wa Kata ya Usevya Halmashauri ya Mpimbwe wilaya Mlele mkoa wa Katavi wakimsikiliza Mbunge wa Jimbo la Kavuu na Naibu Waziri wa Ardhi,Mheshimiwa Geophrey Pinda wakati wa sherehe za kuelekea siku ya wanawake duniani inayoadhimishwa kila mwaka mwezi Machi.

‘’Tukijitangaza mbali zaidi, wafanyabiashara wote watajua twendeni Mpimbwe, mnakumbuka akina mama tumetoka mbali na sasa tunakoelekea Tanzania nzima watu waliobahatika kuzalisha mahindi nchi nzima ni Kavuu,’’ alisema Mbunge huyo wa Jimbo la Kavuu.

Amewataka wanawake hao kutouza mazao kwa papara kwa kuwa ana uhakika bei inaenda kupanda iwapo mazoa yanayozalishwa kwenye halmashauri hiyo yatakapotangazwa ipasavyo kupitia redio jamii ya Mpimbwe fm.
Mkurugenzi wa Halmashauri ya Mpimbwe, Shamim Mwariko alimueleza Mbunge wa Jimbo hilo la Kavuu kuwa, wanawake wa halmashauri hiyo wamejiwekea utaratibu katika kuelekea siku ya wanawake duniani wakutane kila kata na kujadili changamoto zinazowakabili katika maeneo yao.

‘’Mhe, Mbunge leo hapa wanawake wa Usevya wamekutana kufurahi, kusherekea na kula pamoja lakini pia kujadili changamoto zinazowakabili katika maeneo yao,’’ alisema Shamim.
Mbunge wa Jimbo la Kavuu na Naibu Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi,Mheshimiwa Geophrey Pinda akiwapungia mkono wanawake wa kata ya Usevya katika halmashauri ya Mpimbwe mara baada ya kumaliza kuwahutubia wakati wa sherehe za kuelekea siku ya wanawake duniani inayoadhimishwa kila mwaka mwezi Machi.

Kituo cha Redio cha Mpimbwe Fm kinachomilikiwa na halmashauri ya Mpimbwe kimezinduliwa tarehe 25 Februari 2024 na Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mhe, Kassim Majaliwa Majaliwa ambapo aliitaka halmashauri ya Mpimbwe kuitumia redio hiyo kutangaza shughuli za idara kwa wananchi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

2 Comments

Previous Post Next Post

International news