ZANZIBAR-Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imeendesha mafunzo maalum kuhusu uwekezaji katika dhamana za Serikali kwa maofisa wa juu wa Jeshi la Polisi visiwani Zanzibar, wakiongozwa na Mkuu wa Utawala na Rasilimali Watu wa Jeshi hilo Kamisheni ya Zanzibar, Naibu Kamishna wa Polisi (DCP) Simon Thomas Chillery.
Lengo kuu la mafunzo haya ni kuwajengea uwezo na kutoa uelewa mpana juu ya fursa zilizopo katika uwekezaji wa dhamana za Serikali, pamoja na manufaa yake.Mafunzo hayo yaliongozwa na Mkurugenzi wa Tawi la Benki Kuu Zanzibar, Bw. Ibrahim Malogoi, ambapo maofisa hao walielezwa kwa kina kuhusu aina mbalimbali za dhamana za Serikali kama vile hati fungani (treasury bonds) na dhamana za muda mfupi (treasury bills), namna ya kuwekeza na utaratibu wa kushiriki kwenye minada ya dhamana.
Dhamana za Serikali zimeelezwa kuwa ni njia salama na yenye uhakika ya uwekezaji, si kwa taasisi pekee bali pia kwa watu binafsi.
Kupitia uwekezaji huu, wawekezaji hupata riba ya uhakika inayosaidia kuongeza kipato chao, kuimarisha uwezo wao wa kifedha na kukuza uchumi wao binafsi.

