Ajali ya Daladala yaua sita na kujeruhi 21 Sumbawanga

RUKWA-Watu sita wamefariki dunia na wengine 21 kujeruhiwa baada ya daladala yenye namba za usajili T 294 DSS inayofanya safari zake kati ya vijiji vya Sikaungu-Malonje wilayani Sumbawanga kuigonga pikipiki ya magurudumu matatu maarufu kama bajaji.
Ni yenye namba za usajili MC 416 BZQ iliyokuwa imeegeshwa kando ya barabara katika eneo la Ulinji nje kidogo ya mji wa Sumbawanga.

Kamanda wa Polisi Mkoa wa Rukwa, Kamishna Msaidizi wa Polisi, Shadrack Masija amethibitisha kutokea kwa ajali hiyo ambayo taarifa za awali zinaonesha kuwa, ilisababishwa na hitilafu katika mfumo wa breki au dereva kutumia mwendo huru (neutral) katika eneo hatarishi lenye mwinuko mkali.
Mganga Mfawidhi wa Hospitali ya Rufaa ya Mkoa Sumbawanga, Dkt.Ismail Macha ameeleza kuwa, wamepokea milii ya watu sita waliofariki katika ajali hiyo, watu wazima watatu, wanaume wawili, mwanamke mmoja na watoto watatu wa kiume wawili na wa kike mmoja.

Sambamba na majeruhi 21 wakiwemo wanawake 8 na wanaume 13 huku watatu kati yao wakiwa katika hali ya mahututi katika wodi ya uangalizi maalum (ICU).

Mheshimiwa Charles Makongoro Nyerere,Mkuu wa Mkoa wa Rukwa ametoa salamu za pole kwa familia zote za wafiwa, ndugu,jamaa na marafiki wa wahanga wote na kuwatakia uponyaji wa haraka majeruhi wote.
Amewataka madereva kuacha uzembe, ulevi na kuzingatia Sheria za usalama barabarani huku wakihakikisha kuwa vyombo wanavyoviendesha viko katika hali bora kiusalama na vinafaa kwa matumizi wakati wote.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news