NA DIRAMAKINI
BEI za mafuta zinazotumika nchini kuanzia leo Septemba 3, 2025 zimeonesha kuendelea kupungua kwa kwa shilingi 36 kwa petroli na shilingi 23 kwa dizeli kwa mafuta yaliyopokelewa Bandari ya Dar es Salaam, Tanga na Mtwara mtawalia.
Hayo ni kwa mujibu wa taarifa iliyotolewa na Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Udhibiti wa Huduma za Nishati na Maji (EWURA), Dkt.James Andilile ambapo, taarifa imeonesha kushuka kwa bei ya petroli katika soko la dunia kwa 0.2 %, dizeli kwa 5.5 % na mafuta ya taa kwa 3.5%.
Vilevile, kwa bei za mwezi Septemba, 2025 wastani wa gharama za kubadilisha fedha za kigeni umepungua kwa 3.96%, hali iliyopelekea kupungua kwa bei za bidhaa za mafuta kwa mwezi Septemba 2025.
Aidha, kwa mwezi Septemba 2025, gharama za uagizaji mafuta katika bandari ya Dar es salaam zimeongezeka kwa wastani wa 20.73% kwa petroli, 7.75% kwa dizeli na 2.62% kwa mafuta ya taa; na kwa Bandari ya Tanga zimepungua kwa 12.66% kwa petroli na 12.66% kwa dizeli na kutokuwa na mabadiliko katika Bandari ya Mtwara.
Wafanyabiashara wa rejareja na jumla wa bidhaa za mafuta nchini wanakumbushwa kuuza mafuta kwa bei zilizoidhinishwa na EWURA na yeyote atakayekiuka agizo hili atachukuliwa hatua kali za kisheria.
.jpeg)




