Maafisa Mipangomiji wafundwa kutekeleza majukumu kwa weledi

ARUSHA-Katika kuboresha utendaji kazi na usimamizi wa masuala ya mipangomiji nchini Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi kupitia Idara ya Maendeleo ya Makazi inaendesha kikao kazi kwa Maafisa Mipangomiji wa mikoa ili kujipanga kutekeleza majukumu yao kwa weledi.
Kikao hicho cha siku tatu kinachofanyika mkoani Arusha kuanzia SSeptemba 1,2025 hadi Septemba 3,2025 kinatumika kukumbushana maadili kwa Maafisa Mipangomiji, muongozo wa upangaji na utekelezaji mipango ya uendelezaji miji, umuhimu wa kufanya ukaguzi wa matumizi ya ardhi pamoja na uidhinishwaji kazi za mipango miji kwenye mfumo wa e-ardhi.
Idara ya Maendeleo ya Makazi moja ya majukumu yake ni kupanga miji vizuri pamoja na kusimamia uendelezaji wake (development control).

Mkurugenzi wa Maendeleo ya Makazi Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, Bw. Deogratias Kalimenze amewaambia washiriki wakati wa kufungua kikao hicho kuwa, Maafisa Mipangomiji ndiyo waliobeba dhamana nzito ya kuhakikisha ulimwengu unakuwa na sehemu salama ya kuishi.
‘’Tumepewa dhamana ya kuhakikisha kwamba tunawafanya watu waishi katika mazingira ambayo ni mazuri, ni mipango yetu ndiyo inayoongoza namna gani watu wataishi, watafanya kazi, ajira zitakavyopatikana, tutalindaje rasilimali zitumike kizazi na kizazi, nishati itumikeje,’’amesema Kalimenze.

Kwa mujibu wa Mkurugenzi huyo wa Idara ya Maendeleo ya Makazi Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi, upangaji wa miji ni jukumu ambalo watendaji hao wamepangiwa na Mwenyezi Mungu waweze kuilinda dunia na kuwa endelevu.
"Jukumu mlilokuwa nalo Maafisa Mipangomiji nchini ni kubwa na katika kulitekeleza hilo ni lazima muwe na weledi wa hali ya juu, nidhamu katika kutekeleza majukumu pamoja na kuzingatia sheria, kanuni na taratibu zilizowekwa kwa ajili ya kuongoza utekelezaji majukumu ya kila siku ili msisababishe ajali kwa wale mliopewa majukumu ya kuwafanya waishi katika dunia kwa furaha."

Kupitia kikao hicho, tathmini ya utekelezaji wa Bajeti kwa Mwaka 2024/2025 pamoja na utekelezaji kazi za urasimishaji nchini itafanyika. Aidha, kutakuwa na uwasilishaji mada kuhusiana na mfumo wa utoaji huduma za Bodi ya Usajili wa Wataalamu wa Mipangomiji, kupitia na kujadili rasimu ya kanuni ya viwango vya upangaji na makundi ya matumizi pamoja na namna ya kulinda afya ya akili na umuhimu wa akili hisia katika maeneo ya kazi.

Diramakini

DIRAMAKINI is Tanzanian news media house established to play role in shaping the global agenda through telling true stories by delivering quick and in-depth.Our readers trust our coverage of the issues that matter most to them. Our agenda-setting journalism attracts. Contact us on diramakini@gmail.com OR +255 719 254 464.

Post a Comment

Previous Post Next Post

International news