KAGERA-Mahakama ya Wilaya ya Muleba mkoano Kagera leo Septemba 25,2025 imemuhukumu, Bw. Elbert Rutahwa Charles ambaye alikuwa mkusanya mapato ya Halmashauri ya Wilaya ya Muleba baada ya kupatikana na hatia ya kujipatia fedha kwa njia ya rushwa.
Katika shauri la rushwa namba 12/2025, mbele ya Hakimu Mheshimiwa Lilian Mwambelekwa imebainika kuwa, mshtakiwa alijipatia jumla ya shilingi 5,439,700 kupitia mashine ya kukusanyia mapato (POS), fedha ambazo hakuzifikisha kwenye akaunti ya halmashauri kama inavyotakiwa kisheria, badala yake alijifaidisha binafsi.Bw. Rutahwa alikuwa anakabiliwa na kosa la rushwa kinyume na Kifungu cha 15(1)(a) & (2) cha Sheria ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (PCCA) Sura ya 329, marejeo ya mwaka 2023.
Baada ya kutiwa hatiani, Mahakama imemhukumu kulipa faini ya shilingi 500,000 au kifungo cha miaka mitatu jela, pamoja na agizo la kurejesha kiasi chote alichojilimbikizia cha shilingi 5,439,700 ndani ya miezi sita kwa Halmashauri ya Muleba.
Kwa kuwa hakuweza kulipa faini hiyo, Bw. Rutahwa amekwenda jela kutumikia kifungo hicho.
Aidha, shauri hili liliendeshwa na Mwendesha Mashtaka kutoka Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa Tanzania (TAKUKURU) Wilaya ya Muleba, Bw. Mustafa Mcharazo.
Tags
Breaking News
Habari
Mahakamani Leo
Taasisi ya Kuzuia na Kupambana na Rushwa (TAKUKURU)
TAKUKURU