ZANZIBAR-Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Mhe. Dkt. Hussein Ali Mwinyi ameipongeza Klabu ya Young Africans Sports Club kwa ushindi wa bao 1–0 dhidi ya AS FAR Rabat ya Morocco, katika mchezo wa Ligi ya Mabingwa Afrika uliochezwa Novemba 22,2025 katika Uwanja wa New Amaan Complex, Zanzibar.
Amesema kuwa, ushindi huo umeiletea nchi heshima ya kipekee na kuandika ukurasa mpya katika historia ya michezo nchini, huku Young Africans ikionesha kiwango cha juu cha ubunifu, nidhamu na ukomavu wa mchezo uliowezesha kupata matokeo chanya.
Rais Dkt. Mwinyi ameongeza kuwa Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar itaendelea kushirikiana na wadau mbalimbali wa michezo ili kuimarisha miundombinu na mazingira ya michezo nchini, hatua ambayo itaziwezesha timu za ndani kuongeza ushindani na kufanya vizuri katika mashindano ya Kimataifa.
Aidha, Mhe. Rais amewashukuru mashabiki na wananchi wote waliojitokeza kwa wingi kuipa nguvu Young Africans SC, akisema kuwa umoja, hamasa na mshikamano waliouonesha leo umeufanya Uwanja wa New Amaan Complex kuwa sehemu ya historia muhimu katika safari ya kuendeleza michezo nchini.

