PWANI-Januari 08,2026 Mahakama ya Hakimu Mkazi Kibaha imemhukumu Stephano Anyosisye Mwasala (35) mkazi wa Msongola, Kibaha aliyekuwa mmiliki wa kituo cha kulelea watoto wanaoishi kwenye mazingira magumu kiitwacho Majest Children Home kifungo cha maisha jela.
Ni kwa kosa la kuanzisha kituo hicho bila kuwa na leseni,kubaka na kuwanyanyasa kingono watoto saba kati ya aliokuwa anawalea kituoni hapo.Kwa nyakati tofauti kati ya mwezi Disemba 2024 na Januari, 2025 huko Msongola katika kituo hicho cha Majest ilidaiwa mshtakiwa amekua akiwaingilia kimwili na kuwafanyia vitendo vya kingono watoto hao saba wenye umri wa kuanzia miaka 10 hadi 14.
Imeelezwa mahakamani hapo na upande wa Jamhuri kuwa, Jeshi la Polisi mara baada ya kupata taarifa hizo kwa kushirikiana na Ustawi wa Jamii walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa huyo na upelelezi uliendelea kisha mtuhumiwa alifikishwa mahakamani kujibu tuhuma zinazomkabili.
Akisoma hukumu kwa mtuhumiwa, Hakimu Mkazi Mfawidhi wa Mahakama hiyo, Mhe. Joyce Mkhoi alieleza kuwa, Stephano anashtakiwa kwa kosa la kuanzisha kituo bila kuwa na leseni kinyume na kifungu namba 146 (2) (a) cha Sheria ya mtoto, Sura namba 13 ya mwaka 2019 na makosa ya kubaka kinyume na kifungu namba 130 (1), 2 (e) na 131 (1) cha Sheria ya kanuni ya Adhabu, Sura ya 16, Marejeo ya mwaka 2022.
Mshtakiwa amehukumiwa kifungo hicho cha jela maisha ili iwe fundisho kwa wengine wanaovunja sheria za nchi na wanaojihusisha na vitendo vya kikatili kwa watoto na makundi mengine katika jamii.