ARUSHA-Wito umetolewa kwa wananchi kuepuka makundi yanayolenga kuchafua amani na utulivu uliopo nchini, kwani serikali kupitia vyombo vya ulinzi na usalama ipo macho muda wote kuhakikisha inawachukulia hatua za kisheria wote wanaokiuka sheria na taratibu za nchi.
Wito huo umetolewa leo na Mkuu wa Polisi Jamii Wilaya ya Longido, Mrakibu wa Polisi SP Tausi Mbalamwezi katika Kata ya Ngereani wilayani humo ambapo amewahimiza wananchi hususani vijana kuepuka kujiingiza katika makundi yanayolenga kuchafua amani na utulivu uliopo nchini badala yake wajikite katika kufanya kazi kwa bidii katika kuboresha maslahi yao na taifa kwa ujumla.
SP Mbalamwezi pia amewasisitiza wananchi hao kupuuzia taarifa za uchochezi hususani katika mitandao ya kijamii kwani taarifa hizo zimekuwa zikiandaliwa na kusambazwa na wahalifu wasio na nia njema kwa taifa, huku akiongeza kuwa Jeshi la Polisi linaendelea kuwachukulia hatua za kisheria wote wanaobainika.
Aidha, Mkuu huyo wa Polisi jamii amewataka vijana wa kata hiyo kushiriki katika bonanza la michezo la Amani Cup lililoandaliwa na Jeshi Polisi ili kuimarisha ushirikiano uliopo kati ya jamii na Jeshi la Polisi katika kubaini na kutokomeza Uhalifu.
