DAR-Serikali kupitia Wizara ya Afya imefanya mazungumzo na Shirika la Ushirikiano wa Kimataifa la Korea (KOICA) kwa ajili ya kujadili ushirikiano wa utekelezaji wa mradi wa kuimarisha huduma za uangalizi mahututi kwa kwa hospitali za rufaa jijini Dar es Salaam wenye dhamani ya dola za Marekani millioni 14.5.
Katibu Mkuu wa Wizara ya Afya, Dkt. Seif Shekalaghe akiongea Februari 3, 2026, katika ofisi za Wizara jijini Dar es Salaam amesema mradi huo.unatarajiwa kutekelezwa katika hospitali tatu za rufaa za mikoa ambazo ni Hospitali ya Rufaa ya Amana, Mwananyamala na Temeke.
Dkt. Shekalaghe amesema mradi pia unalenga kuboresha mifumo ya rufaa za dharura na usafirishaji wa wagonjwa kwa kununua ambulensi nane, kati ya hizo, hospitali za Amana, Mwananyamala na Temeke zitapokea ambulensi tatu kila moja, huku ambulensi mbili zikitengwa kwa ajili ya kuunga mkono mradi wa usafiri wa dharura wa m-Mama.
Katika kikao hicho, KOICA imewasilisha maelezo ya kina kuhusu wigo na malengo ya mradi, ambapo maeneo makuu ya utekelezaji yameainishwa kuwa ni pamoja na kuanzishwa kwa vituo vya uangalizi mahututi (ICU) kwa akina mama na watoto wachanga walio katika hatari kubwa katika Hospitali za Rufaa za Amana na Mwananyamala.
Aidha, mradi utahusisha ununuzi na usambazaji wa vifaa tiba vya kisasa kwa ajili ya huduma za uzazi na watoto wachanga katika hospitali zote tatu, pamoja na kujenga uwezo wa watumishi wa afya kupitia mafunzo maalum ya kuimarisha utoaji wa huduma za uangalizi mahututi.
