■Asema Dkt.Samia amewapa elimu kuwa urithi watoto wa Kitanzania
KILIMANJARO-Waziri Mkuu Dkt.Mwigulu Nchemba amewataka wanafunzi wanaosoma shule ya sekondari ya wasichana ya mkoa wa Kilimanjaro wasome kwa bidii ili kuwaenzi wazazi wao pamoja na jitihada za Rais Dkt. Samia Suluhu Hassan.
“Wanangu someni kwa bidii, kitu pekee cha kuwalipa wazazi wenu na furaha tutakayompa Dkt.Samia Suluhu Hassan ni kufaulu vizuri sana,” amesisitiza wakati akiongea na wanafunzi zaidi ya 600 wa shule hiyo pamoja na wananchi waliofika kushuhudia uwekaji wa jiwe la msingi uliofanyika leo Februari 21, 2026 kwenye shule hiyo iliyopo katika Kijiji cha Mawasiliano, Kata ya Gararagua wilayani Siha.
“Nilipofika hapa Kilimanjaro Girls’ nilifurahi kusikia kwamba ni shule ya masomo ya sayansi tena ina tahsusi ya PCM. Hii imenifanya nikumbuke pure mathematics inayoanza na quadratics, inakuja functions, inakuja coordinate geometry ... na tunamaliza na calculus, differentifation and integration,” alitaja baadhi ya topics huku akishangiliwa na wanafunzi hao.Aliwasisitiza wanafunzi hao wafanye bidii kwenye masomo na kuhakikisha wanafika vyuo vikuu.
"Mwanafunzi soma kwa bidii, usiruhusu kufika level hii halafu ukakosa kwenda chuo kikuu au chuo kingine cha elimu ya juu. Rais Dkt. Samia amewapa elimu watoto wa Kitanzania kwa kuwatengenezea urithi wa aina hii,” alisema.
Kwa mujibu wa taarifa ya ujenzi iliyotolewa mbele ya Waziri Mkuu, sh. bilioni 4.45 zilipokelewa kwa ajili ya ujenzi wa madarasa 22, mabweni 12, jengo la utawala moja, bwalo moja, nyumba za watumishi nane na maabara nne.
Vingine ni chumba cha TEHAMA kimoja, maktaba moja, chumba cha wagonjwa kimoja, chumba cha jenereta kimoja na matundu 16 ya choo. Ujenzi bado unaendelea na umefikia asilimia 85.04.


