MWANZA-Mkuu wa Dawati la Jinsia na Watoto Wilaya ya Ilemela mkoani Mwanza, Mkaguzi wa Polisi, Kulwa Mcha, akiwa ameambatana na SGT Jeremiah Makoromu, Februari 27,2026, walitoa elimu ya kuzuia uhalifu kwa wanafunzi wa Shule ya Msingi Ibungilo, kwa lengo la kupinga ukatili na unyanyasaji wa watoto.
Elimu hiyo imelenga kuwajengea uwezo wanafunzi kuelewa haki zao za msingi kisheria, kutambua vyanzo vya ukatili, pamoja na mbinu madhubuti za kuzuia vitendo hivyo katika mazingira yanayowazunguka.
Akizungumza na wanafunzi hao, Mkaguzi Mcha amewataka kuvunja ukimya kwa kutoa taarifa mapema pindi wanapokutana na viashiria vya unyanyasaji, akibainisha kuwa kuficha vitendo hivyo huongeza madhara kwa mwathirika na kutoa mwanya kwa wahalifu kuendelea na vitendo vyao.
Aidha, aliwakambusha kuchukua tahadhari ya kiusalama kutokana na madhara yanayoweza kujitokeza kutokana na mvua zinazoendelea kunyesha hasa wanafunzi hao wanapokuwa njiani kuelekea au kurudi shuleni ili kuepuka majanga yanayoweza kuzuilika.
Hatua hii ni muendelezo na sehemu ya mikakati ya Jeshi la Polisi katika kulinda raia na mali zao huku likihakikisha mazingira ya elimu kwa watoto yanakuwa salama na kumwezesha mwanafunzi kukua na kutimiza ndoto zake bila bughudha.