DAR-Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), ameshiriki Futari iliyoandaliwa na Benki ya NMB katika ukumbi wa SuperDome, jijini Dar es Salaam.
Hafla hiyo imewakutanisha viongozi wa serikali, sekta binafsi, wadau wa maendeleo na baadhi ya wakazi wa jiji la Dar es Salaam kwa lengo la kuimarisha ushirikiano na kuendeleza umoja wa kitaifa katika kipindi hiki cha Mwezi Mtukufu wa Ramadhani.
Katika tukio hilo, Mhe. Balozi Omar pia alikabidhi zawadi kwa watu wenye mahitaji maalum walioko katika baadhi ya vituo vya kulelea watoto kama ishara ya upendo, mshikamano na utu wema unaohimizwa katika kipindi cha Ramadhani.
Mheshimiwa Balozi Omar aliwapongeza NMB kwa mchango wao katika jamii na kuendelea kusaidia juhudi za Serikali katika kuinua maisha ya wananchi na akatoa wito kwa taasisi, kampuni, mashirika na wadau wengine kuiga utamaduni wa NMB wa kutambua mchango wa wadau wao na kuonesha upendo.














