DAR-Benki Kuu ya Tanzania (BoT) imepongezwa kwa usimamizi wake thabiti wa sekta ya kibenki, hali inayochangia kuongezeka kwa faida za mabenki nchini pamoja na kukuza ustawi wa sekta ya fedha kwa ujumla.
Pongezi hizo zimetolewa na Afisa Mtendaji Mkuu wa NCBA Group Kenya, Bw. John Gachora, alipotembelea Benki Kuu tarehe 30 Machi 2026 na kufanya mazungumzo na Gavana wa BoT, Bw. Emmanuel Tutuba. Mazungumzo hayo yalilenga kujadili dhamira ya Nedbank Group Limited kununua asilimia 66 ya hisa za NCBA Group Limited.“Naipongeza BoT kwa usimamizi mzuri wa sekta ya kibenki. Ukiangalia takwimu, utagundua kuwa kuna ongezeko la faida kwa mabenki nchini kila mwaka. Hii inatokana na usimamizi madhubuti wa BoT pamoja na uwepo wa mazingira rafiki kwa mabenki kufanya shughuli zao.”
Aidha, amesisitiza kuwa Benki Kuu itaendelea kuweka mazingira wezeshi ili kuhakikisha mabenki yanaendelea kustawi. Pia alihimiza mabenki kutumia fursa ya upatikanaji wa umeme wa uhakika na kuimarika kwa teknolojia ya intaneti ili kubuni huduma za kidijitali zitakazoongeza ufanisi na kupanua upatikanaji wa huduma za kifedha kwa wananchi.
Hadi kufikia tarehe 31 Desemba 2025, Tanzania ilikuwa na jumla ya benki 42 zilizosajiliwa. Kati ya hizo, 35 ni benki za biashara, tatu ni benki za huduma ndogo za fedha, mbili ni benki za jamii, na mbili ni benki za maendeleo.



