ZANZIBAR-Naibu Katibu Mkuu wa Chama Cha Mapinduzi Zanzibar, Dkt. Mohammed Said Mohammed (DIMWA) ameshiriki kama mgeni rasmi katika fainali za mashindano ya Morgan & Shebi Cup zilizofanyika Machi 19,2026 katika viwanja vya Migombani, Zanzibar.

Akizungumza katika hafla hiyo, Dkt. Mohammed amewahimiza wananchi kuendelea kushirikiana kwa karibu na viongozi wa majimbo yao ili kuharakisha utekelezaji wa shughuli za maendeleo katika maeneo yao. Amesisitiza kuwa, ushirikiano huo ni nguzo muhimu katika kufanikisha mipango ya kijamii na kiuchumi.
Mashindano hayo, yaliyoandaliwa kwa ushirikiano kati ya Mbunge na Mwakilishi wa Jimbo la Mpendae, yamelenga kukuza vipaji vya michezo kwa vijana pamoja na kuimarisha mshikamano wa kijamii miongoni mwa wananchi.
Katika hotuba yake, Dkt. Mohammed pia amepongeza juhudi za Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, ambaye pia ni Rais wa Zanzibar na Mwenyekiti wa Baraza la Mapinduzi, Dkt. Hussein Ali Mwinyi, kwa kuendelea kuimarisha miundombinu ya michezo nchini.
Amesema kuwa, ujenzi wa viwanja vya kisasa unatoa fursa kwa vijana kuendeleza vipaji vyao na kuinua kiwango cha michezo.
















