DODOMA-Waziri wa Fedha Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb), amewataka watumishi wa wizara hiyo kuzingatia uadilifu katika kazi zao za kila siku, akisisitiza kuwa uadilifu ni matakwa ya Mwenyezi Mungu na si jambo la msimu wa mfungo pekee.
Mhe. Balozi Omar aliyasema hayo wakati akihutubia jijini Dodoma katika hafla ya futari maalum iliyoandaliwa na Idara ya Mhasibu Mkuu wa Serikali, ikiongozwa na CPA Leonard Mkude, kwa watumishi wa Wizara ya Fedha.

Alieleza kuwa, maadili ya kazi ni msingi wa uwajibikaji na uaminifu na yanapaswa kudumu muda wote ili kuimarisha imani ya wananchi kwa Serikali na taasisi zake.
Alibainisha kuwa,ushirikiano wa dhati ni chachu ya kusukuma gurudumu la maendeleo ya Taifa, kwa kuwa kila mtumishi anapaswa kutambua nafasi yake katika kufanikisha malengo ya wizara na Serikali kwa ujumla.Alisisitiza kuwa, watumishi wa wizara ya fedha wanapaswa kuwa mfano wa uadilifu na ushirikiano, akieleza kuwa maadili bora ya kazi ndiyo msingi wa maendeleo endelevu na ustawi wa Taifa.
Kwa upande wake, Naibu Waziri wa Fedha, Mhe. Mshamu Ali Munde, alisema kuwa tukio hilo la futari linaonesha jinsi Tanzania ilivyo na umoja na mshikamo licha ya kuwa na dini ama madhehebu mbalimbali.
Halfa hiyo ilihudhuriwa pia na Kaimu Katibu Mkuu Naibu Katibu Mkuu, Wizara ya Fedha, Bw. Elijah Mwandumbya na Sheikh Mkuu wa Mkoa wa Dodoma Alhaj Mustapha Rajab Shaban.








