DAR-Waziri wa Fedha, Mhe. Balozi Khamis Mussa Omar (Mb) amethibitisha dhamira ya serikali chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuendelea kuimarisha ushirikiano wake na Canada ili kufikia malengo endelevu na ustawi wa wananchi kiuchumi, kijamii na kisiasa.
Mhe. Balozi Omar amesema hayo, alipokutana na kufanya mazungumzo na Balozi wa Canada nchini Tanzania, Mhe Emily Burns, katika Ofisi Ndogo za Wizara ya Fedha jijini Dar es Salaam.Alisema kuwa, Serikali ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania na Serikali ya Canada zimeimarisha ushirikiano wao wa maendeleo unaolenga sekta za afya, elimu na maendeleo ya kijamii na kiuchumi.
Alisema kuwa ushirikiano wa Canada katika sekta muhimu kama kilimo, elimu, afya, ukuaji wa uchumi na ulinzi wa jamii umechangia kwa kiasi kikubwa katika mageuzi ya kijamii na kiuchumi ya Tanzania.
“Tuko tayari kushirikiana kwa karibu zaidi ili kuimarisha uhusiano wetu wa maendeleo na tunatarajia kuona fursa mpya zitakazonufaisha wananchi wetu kwa kuwekeza katika sekta mbalimbali za kiuchumi na kibiashara na tumeendelea kuboresha mazingira ya uwekezaji na biashara, hivyo tunawakaribisha wawekezaji nchini,” alisisitiza Mhe. Balozi Omar.
Aidha, alithibitisha dhamira ya Serikali ya Tanzania, chini ya uongozi wa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Mhe. Dkt. Samia Suluhu Hassan, kuendelea kuimarisha ushirikiano huo kwa lengo la kufikia maendeleo endelevu na ustawi wa wananchi.
Kwa upande wake, Balozi wa Canada nchini Tanzania alisifu ushirikiano wa kidiplomasia na kiuchumi kati ya Tanzania na nchi yake na kueleza kifurahishwa na mafanikio ya Tanzania katika nyanja mbalimbali.Alisema wawekezaji wengi wanavutiwa na mazingira bora ya ufanyaji biashara na uwekezaji nchini na kuishauri Serikali kufanyiakazi kwa uharaka mkataba wa kutotoza kodi mara mbili na kuzuia ukwepaji kodi kati ya nchi hizo mbili.
Kikao hicho kilihuhudhuriwa pia na Katibu Mkuu wa Wizara ya Fedha, Dkt. Natu El-maamry Mwamba, maafisa waandamizi kutoka Wizara ya Fedha na Ofisi ya Rais Mipango na uwekezaji, Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, na wawakilishi wa Ubalozi wa Canada.
