DODOMA-Wizara ya Fedha imeungana na Watanzania wengine kuadhimisha Siku ya Kimataifa ya Wanawake Duniani kwa kutoa elimu ya fedha ili kuwawezesha wanawake na jamii kufikia uhuru wa kifedha.
Maadhimisho hayo yamefanyika katika viwanja vya Shule ya Msingi Mbande wilayani Kongwa mkoani Dodoma yakiwa na kauli mbiu “Haki na Usawa kwa Wanawake na Wasichana: Msingi Jumuishi kufikia Dira 2050”, ikilenga kujenga uelewa wa kuwekeza katika maendeleo jumuishi kwa kutambua na kutekeleza haki za wanawake na wasichana kwa vitendo.
Wizara ya Fedha ilitoa elimu kwa umma kuhusu usimamizi wa fedha binafsi, umuhimu wa kuweka akiba, umuhimu wa kutumia huduma rasmi za fedha na umuhimu wa kutumia bima.








